Macho yote ni Twiga Stars leo Botswana
KOCHA Mkuu wa Twiga Stars, Bakar Shime amesema wachezaji wa timu hiyo wako vizuri kuwakabili Botswana kwenye mchezo wa marudiano kufuzu michuano ya Olimpiki mwakani nchini Ufaransa.
Mchezo wa kwanza Stars ilishinda mabao 2-0 yaliyofungwa na Opah Clement na Aisha Masaka na mchezo wa pili utachezwa leo Gaborone nchini Botswana.
Stars ilianza hatua ya pili michuano hiyo baada ya Brazaville kujitoa na ikishinda mchezo wa pili itatinga raundi ya tatu itakutana na mshindi kati ya DR Congo na Afrika Kusini ambao kwenye mechi ya kwanza walitoka sare ya bao 1-1.
Shime alisema jana asubuhi kikosi kilifanya mazoezi mepesi ya Gym kuweka mwili sawa na jioni walifanya mazoezi kiwanjani hivyo kwa asilimia kubwa wako tayari kwa mchezo.
Aliongeza kuwa kuna majeruhi wachache kama Amina Ally lakini kwa sasa wanaendelea vizuri na wakiamka salama wataanza kwenye mechi hiyo.
“Kuna baadhi ya wachezaji walipata majeraha wengine hawakucheza kabisa mechi ya Dar lakini sasa wako fiti naamini wataanza kwenye mechi ya leo,”alisema Shime.