Mabingwa Mtambile Jimbo Cup wajazwa noti

Mbunge wa Mtambile, Seif Salim Seif (kulia) akimkabidhi kikombe cha ushindi wa kwanza nahodha wa timu ya Juhudi baada ya kushinda mashindao ya Jimbo. Mbali ya kikombe, timi hiyo pia ilizawadiwa Sh1 milioni.
Mbunge wa Mtambile, Seif Salim Seif amewazadia pesa, vifaa vya michezo na medali washindi wa michuano ya soka ya Mtambile Jimbo Cup yaliyofungwa juzi kwenye uwanja wa Kengeja, mjini hapa.
Timu ya Juhudi ilitawazwa kuwa ubingwa msimu huu baada ya kuifunga Mizingani mabao 2-0. kwenye mashindano hayo yaliyoshirikisha timu 20.
Kwa ushindi huo, Juhudi ilizawadiwa, kikombe, na pesa Taslimu Sh 1Milioni, medali ya dhahabu na mipira 10 kutoka kwa Seif ambaye ni Mbunge kupitia Chama Cha Wananchi (CUF).
Mbali ya kutwaa kombe, mchezaji Hafidhi Ali Maalim wa timu hiyo alishinda tuzo ya mchezaji bora wa mashindano na kuzawadiwa kiatu chenye thamani ya sh100,000.
Mshindi wa pili timu ya Mizingani ilizawadiwa Sh500,000, mipira mitano na jezi seti moja wakati mshindi wa tatu timu ya Maendeleo ilizawadiwa Sh300,000, jezi seti moja na mipira mitatu.
Timu ya Warriors ilimaliza ya nne na kuzawadiwa Sh200,000, jezi seti moja na mipira miwili huku timu Mtadoda FC ilizawadiwa Sh250,000 na mipira miwili kwa kuwa timu yenye nidhamu.
Akizungumza wakati wa ufungaji wa mashindano hayo, Seif alisema kuwa mbali ya kuendeleza mpira wa miguu, mashindano hayo pia yana lengo la kudumisha umoja na kutafuta wachezaji wa kuunda timu ya Jimbo lake ambayo itashiriki katika mashindano mbalimbali.
Alisema kuwa mpaka sasa amevutiwa na wachezaji wengi wenye vipaji ambao wanatakiwa kuendelezwa ili kufikia kiwango cha kuchezea timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars).
“Malengo yamefanikiwa kwani kupitia mashindano haya, tumeweza kuwa pamoja na kushikamana mbali ya kushindana kupitia timu zetu, nazipongeza timu shiriki, mashabiki na viongozi walioshiriki kufabikisha mashindano haya,” alisema Seif.