Dickson Job ajutia kifungo

KIFUNGO cha kutocheza mechi tatu alichopewa beki wa Yanga, Dickson Job kutoka Bodi ya Ligi kupitia Kamati ya Saa 72 imemvuruga beki huyo na kujutia makosa yake.
Job alimkanyaga nyota wa Mbeya City, Richardson Ng’ondya na ndipo Kamati ya 72 ikampiga kifungo cha kutocheza mechi tatu ikiwamo ya kesho ya Kombe la Shirikisho la Azam Sports (ASFC) dhidi ya Biashara United na mbili za Ligi Kuu Bara dhidi ya Mtibwa Sugar na Kagera Sugar.
Mbali na kuzikosa mechi hizo, lakini beki huyo wa kati ambaye kwa siku za karibuni amekuwa akitumika kama beki wa kulia wa Yanga, amelimwa pia faini ya Sh 500,000 na kumfanya ajutie kosa akimuomba radhi Ng’ondya.
“Inaniuma sana, sikudhamiria kufanya vile. Ilitokea tu kama ajali katika mchezo na nimemuomba radhi Ng’ondya na jamii ya wanamichezo wote kwa ujumla, sitarudia kosa kama lile,” alisema Job na kuongeza;
“Kupitia tukio lile nimejifunza, nitaendelea kufanya mazoezi na nikirejea uwanjani naamini nitakuwa bora na kucheza kwa kwa kuzingatia afya ya wachezaji wenzangu.”
Katika mchezo huo baina ya timu zao, dakika 90 ziliisha kwa suluhu, huku Yanga ikinyimwa bao la wazi baada ya waamuzi kutafsiri Fiston Mayele alikuwa ameotea japo marudio ya Azam TV yaliwaumbua na marefa hao waliondolewa katika orodha ya kuchezesha Ligi Kuu.