Dejan bye bye Simba, akaa siku 54

ALIYEKUWA Mshambuliaji wa Simba Mserbia, Dejan Georgijevic amethibitisha kuvunja mkataba na miamba hiyo ikiwa ni muda mfupi tangu alipojiunga nao.

Nyota huyo aliyesajiliwa na Kocha Zoran Maki ambaye naye aliondoka na kutimkia Misri alijiunga na Simba Agosti 7 mwaka huu akitokea NK Domzale ambapo tangu ametua nchini amekuwa gumzo kubwa kutokana na kuwavutia mashabiki.

Kupitia mtandao wake wa kijamii wa Instagram Dejan aliandika; "Nathibitisha mkataba wangu na waajiri wangu umevunjika, asanteni sana mashabiki kwa sapoti na mapenzi mliyonipa,"

Nyota huyo anaondoka kwenye kikosi hicho akiwa amefunga bao moja tu kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Kagera Sugar Agosti 20, wakati Simba iliposhinda mabao 2-0, mechi iliyopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa.