Beki awachanganya Wabrazili Yanga

Jaja na Countinho
Muktasari:
Mchezaji huyo alikuwa hapewi nafasi kwenye kikosi hicho mpaka alipoumia Oscar Joshua ambaye Maximo alikuwa akimuamini zaidi kutokana na uzoefu na rekodi zake.
KIWANGO na ubunifu wa beki wa kushoto wa Yanga, Edward Charles umewakolea makocha wa timu hiyo na sasa ana uwezekano mkubwa wa kucheza mechi nyingi kwenye kikosi cha kwanza.
Mchezaji huyo alikuwa hapewi nafasi kwenye kikosi hicho mpaka alipoumia Oscar Joshua ambaye Maximo alikuwa akimuamini zaidi kutokana na uzoefu na rekodi zake.
Kocha Msaidizi wa Yanga Leonardo Neiva alisema: “Tutampa nafasi Charles, anaweza kupandisha mashambulizi kwa kuwa ana spidi nzuri hiyo ni faida kwetu na mfumo tutakaokuwa tukiutumia. Oscar Joshua naye atakuwa na nafasi kulingana na mchezo lakini pia ubora alionao utahitajika wakati fulani.”
Awali kabla ya kuanza kwa ligi Maximo na benchi lake la ufundi waliwahi kuwapa mazoezi Yanga jinsi ya kupiga krosi na kuzuia na kumalizia mipira ya kona.
Wiki hii kwenye mazoezi walianza zoezi hilo na kocha Neiva alisema sababu kubwa ni kurekebisha makosa madogo yaliyokuwa yanayoonekana kwenye eneo hilo.
“ Tumeangalia zaidi umaliziaji wa mipira inayotokana na kona lakini pia jinsi ya kuzuia, imetulazimu kufanya hivyo ili kuwe na ufanisi wa ziada haswa kwenye upigaji pasi.
“Hii itasaidia timu kufanya mambo makubwa kwenye kila mchezo wanaocheza na hapa mchezaji atajua wapi kwa kumpelekea mchezaji mwingine pasi. Soka limekuwa likirudi nyuma kutokana na wachezaji kutojua wapi wanatakiwa kucheza badala yake wamekuwa wakipiga mpira bila mwelekeo wenye faida,” alisema.
Awali Yanga ilikuwa ikitumia mifumo miwili ambayo ni 4-4-2 na 4-3-3 lakini sasa wameachana na mifumo hiyo baada ya kuona timu nyingi zinaitumia. Wamegeukia mifumo ya 4-2-3-1 na 4-1-3-2 ambapo safu ya ulinzi inabaki vile vile huku wakitegemea kumtumia zaidi Edward Charles kwenye beki ya kushoto zaidi kutokana na uwezo wake wa kupandisha mashambulizi.
Kiungo mkabaji atacheza Mbuyu Twite na wakati mwingine atakuwa akisaidiana na Hassan Dilunga huku kwenye safu ya ushambuliaji kutakuwepo na Andrey Coutinho, Genilson Santos ‘Jaja’, Haruna Niyonzima na Mrisho Ngassa.
Kocha Neiva anakiri kuwa kuna mabadiliko wameyafanya kwenye kikosi kipindi cha mazoezi lakini akakiri kuwa watakuwa na kikosi cha kwanza na wakati huo huo kutakuwa na kikosi imara cha benchi.