Banda amaliza utata Simba, Yanga

KLABU ya Big Bullets, imethibitisha kuachana na winga wao Peter Banda baada ya kuanza makubaliano na Simba ambayo imemsajili nyota huyo kwa mkataba wa miaka mitatu.

Muda mchache baada ya uthibitisho wa klabu yake ya zamani, Simba wamemtambulisha winga huyo mpya kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram.

Ujio wa Banda ndani ya Simba unathibitisha kuachwa Perfect Chikwende aliyesajiliwa na Simba akitokea FC Platnumz ya Zimbabwe.

Banda ni mchezaji wa kwanza wa kigeni kusajiliwa na mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2021/22 inayotarajiwa kuiwakilisha nchi kwenye mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Usajili huo unazima tetesi za kutaka kutua Yanga ambazo tangu jana zimekuwa zikienea mtandaoni.