Amaan yachangamka mapema, mashabiki Simba waonyesha vidole vitatu

Muktasari:
- Tangu alfajiri ya leo, Zanzibar imepambwa na jezi zenye rangi nyekundu na nyeupe sambamba na stori za hapa na pale kuhusu fainali hiyo ya CAF ambayo kwa mara ya kwanza inachezwa visiwani humo.
LEO ni siku ya kihistoria katika ardhi ya visiwa vya Zanzibar. Uwanja wa New Amaan, uliopo Unguja umebeba matumaini kwa mashabiki wa Simba, ambao wamefurika kwa maelfu wakiwa na lengo moja tu kushuhudia timu yao ikipindua meza dhidi ya RS Berkane ya Morocco na kutwaa Kombe la Shirikisho Afrika.
Tangu alfajiri ya leo, Zanzibar imepambwa na jezi zenye rangi nyekundu na nyeupe sambamba na stori za hapa na pale kuhusu fainali hiyo ya CAF ambayo kwa mara ya kwanza inachezwa visiwani humo.
Simba ina kibarua cha kupindua matokeo ya 2-0 baada ya kupoteza katika fainali ya kwanza iliyochezwa Berkane.

BARABARA ZAFUNGWA, ZENJI YASIMAMA
Barabara nyingi zinazozunguka Uwanja wa Amaan zimefungwa rasmi kwa ajili ya kuhakikisha usalama na kupokea wageni maalum kutoka sehemu mbalimbali za ndani na nje ya nchi.
Kikosi cha usalama kimewekwa kila kona, huku magari ya doria yakizunguka kuhakikisha kila kitu kinaenda kwa mpangilio.
Mji wa Zanzibar kwa sasa upo bize na fainali tu. Hoteli zimejaa, biashara za jezi, vinywaji, vuvuzela, na bidhaa za Simba zinauzwa kwa kasi isiyo ya kawaida.
Wachoraji wa usoni wamepiga kambi karibu na uwanja, wakichora nyuso za mashabiki kwa rangi za Simba nyekundu na nyeupe.

TUTAPINDUA MEZA, TUNATAKA UBINGWA
Mashabiki wa Simba wameonyesha imani kubwa licha ya timu yao kupoteza kwa mabao 2-0 katika mechi ya kwanza.
Wanaamini, Simba ikicheza mbele ya mashabiki kwenye ardhi ya Tanzania, ndani ya uwanja wa Amaan, hakuna lisilowezekana.
"Tunaamini kabisa tutashinda. Tunahitaji mabao matatu na tutayapata. Hii ni Simba, tunajua kupambana. Leo tunaandika historia mpya," amesema Ally Omary, shabiki mkongwe kutoka Tanga.

Maandalizi yote ya fainali hii yamekamilika. CAF imeridhika na hali ya uwanja, vifaa, taa, usalama na mapokezi. Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika, Dk Patrice Motsepe, anatarajiwa kuhudhuria, sambamba na viongozi wa juu kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, TFF, na mabalozi wa mataifa mbalimbali.
Simba inahitaji ushindi wa mabao 3-0 matatu ili kutwaa taji hilo la kihistoria. Ikiwa watashinda 2-0, mchezo utaenda muda wa nyongeza au mikwaju ya penalti. Hii ni fursa ya kuandika ukurasa mpya wa mafanikio katika historia ya soka la Tanzania.