Al Ahly watua kiuoga

MABINGWA watetezi wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Al Ahly ya Misri wanatua jijini Dar es Salaam leo ila kwa tahadhari kubwa.

Katika kile kinachoonekana ni woga na kuchukua tahadhari kubwa, mashushushu wao walitua Dar es Salaam juzi na jana waliangalia mechi ya Simba na Biashara wakiwa hotelini.

Mwanaspoti linajua kwamba kikosi kizima kitawasili leo Dar es Salaam kwa ndege binafsi tayari kujiandaa na lolote kwenye mechi yao na Simba, Jumanne saa 10 jioni ndani ya Uwanja wa Mkapa.

Kocha wao, Pitso Motsimane ambaye ni Msauzi ameshtushwa na kasi ya Simba hasa baada ya kuipiga AS Vita bao 1-0 ugenini licha ya kwamba wao nao waliitwanga El Merreikh mabao 3-0 nchini Misri.

Motsimane anahofia rekodi za Simba kwenye Uwanja wa Mkapa ambayo imekuwa haipotezi mechi katika miaka ya hivi karibuni.

Al Ahly wanatua na mziki wote wakijiandaa kwa lolote linaloweza kutokea kama baadhi ya mastaa wao wataonekana kuwa na corona, ingawa jana waliwapima wote.