Simba, Yanga kinapigwa usiku

UTAMU wa Ligi Kuu ya Vijana U20, umerudi upya wakati Simba na Yanga zikiliamsha kwenye pambano lao la hatua ya Nane Bora, ngoma ikipigwa leo usiku.

Timu hizo za vijana wa wababe wa soka nchini, litapigwa saa 3:00 usiku, mara baada ya pambano la ufunguzi wa hatua hiyo litakalozikutanisha JKT Tanzania na Mwadui waliopangwa Kundi A sambamba na vigogo hao, mchezo utakaochezwa saa 1:00 usiku.

Timu hizo nane za vijana zilifuzu hatua hii kutoka katika makundi tofauti ya awali yaliyojumuisha jumla ya timu 18 za vijana kutoka timu zinazoshiriki Ligi Kuu U20 na katika upangaji wa makundi hayo ya Nane Bora kusaka timu nne za kucheza nusu fainali Simba na Yanga zikaangukia pamoja.

Simba ilifuzu nane Bora baada ya kumaliza nafasi ya pili katika Kundi B ikiwa na alama 18 baada ya mechi 10, kundi lililokuwa na Mtibwa Sugar, Mwadui, JKT Tanzania, Mbeya City, KMC na Ihefu, wakati Yanga ilimaliza kama kinara wa kundi A ikivuna alama 16, ikizizidi ujanja Azam, Ruvu Shooting, Polisi Tanzania, Coastal Union na Namungo.

Pambano hilo la watani wa jadi hado vijana linasubiriwa kwa hamu hasa baada ya kaka zao kukwepana kwenye mechi yao ya marudiano ya Kariakoo derby ilipokuwa ipigwe Mei 8 kabla ya kuopangwa tena ichezwe Julai 3.

Mechi hiyo pia inatarajiwa kuwa na ushindani wa hali ya juu kutokana na kila timu kutaka alama tatu zitakazofanya imalize nafasi ya mbili za juu kwenye kundi ili kuingia nusu fainali ya michuano hiyo kisha fainali.