Washambuliaji hawajaitendea haki Mashujaa
Muktasari:
- Kwa takwimu za uhakika ambazo kijiwe inazo ni idadi ya mabao yaliyofungwa msimu huu ni 522 ambayo yamepungua kidogo kulinganisha na msimu uliopita na yalifungwa mabao 572.
Msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2025/2026 ulifikia tamati Jumanne iliyopita na Yanga ilitwaa ubingwa baada ya kumaliza ikiwa na pointi 75.
Kwa takwimu za uhakika ambazo kijiwe inazo ni idadi ya mabao yaliyofungwa msimu huu ni 522 ambayo yamepungua kidogo kulinganisha na msimu uliopita na yalifungwa mabao 572.
Timu nyingi zimechangia kuporomoka kwa namba hiyo ya mabao katika msimu uliomalizika kutokana na ubutu wa kufumania nyavu ambao zimeonyesha.
Miongoni mwa zilizochangia kwa kiasi kikubwa ni Mashujaa FC ya Kigoma ambayo imemaliza msimu ikiwa imefunga mabao 15 tu katika mechi 30 za msimu.
Hii maana yake ni kwa wastani, Mashujaa FC ilikuwa inafunga bao 0.5 kwa kila mechi au ilikuwa inapachika bao moja kila baada ya mechi mbili.
Msimu wa 2024/2025, timu hiyo ilipachika mabao 29 hivyo kwa msimu uliomalizika, kuna mabao 14 ambayo yamepungua.
Kuna namna washambuliaji wa Mashujaa FC wameiangusha timu hiyo katika msimu uliomalizika kwa sababu wengi wameonyesha kupoteza makali ya kufumania nyavu licha ya matumaini makubwa ambayo yalikuwepo kwao mwanzoni mwa msimu.
Bahati mbaya ni washambuliaji ambao walichowahi kukifanya hapo nyuma katika timu mbalimbali kiliwapa deni la kuonyesha kitu ndani ya Mashujaa FC katika msimu uliopita.
Washambuliaji kama Dan Lyanga, Richard Ulomi, Japhary Kibaya, Mudathir Said, Ismail Mgunda, Seleman Bwenzi na Salum Kihimbwa kumaliza msimu huku kutokuwepo hata na mmoja kati yao aliyefunga angalau mabao manne sio sawa.