Beckham, Katherine wakutana Wimbledon bila kuzungumza
Muktasari:
- Beckham, 51, alifika kwenye michuano hiyo akiwa ameongozana na mama yake, Sandra huku Katherine 46, akiwa pamoja na mumewe Andrew Levitas.
LONDON, ENGLAND: NYOTA wa zamani wa Man United, David Beckham na mwimbaji wa opera Katherine Jenkinswameingia kwenye vichwa mbalimbali vya habari baada ya wawili hao kukaa karibu kwenye Royal Box wakati wa siku ya ufunguzi wa mashindano ya Wimbledon bila ya kuongeleshana chochote.
Beckham, 51, alifika kwenye michuano hiyo akiwa ameongozana na mama yake, Sandra huku Katherine 46, akiwa pamoja na mumewe Andrew Levitas.
Wawili hao waliketi pamoja hatua chache picha zilionyesha Beckham akifuatilia mchezo huku Katherine akizungumza na wageni wengine waliokuwa eneo hilo.
Mastaa hao hawana maelewano mazuri tangu mwaka 2012 baada ya Katherine kulazimika kukanusha uvumi uliodai alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Beckham. Wakati huo amesema madai hayo hayakuwa ya kweli na yalimuumiza kwa kiasi kikubwa.
Mambo yalikuwa mabaya zaidi mwaka 2017 baada ya kuvuja kwa barua pepe zilizodaiwa kuwa za Beckham, ambazo zilimnukuu akikosoa tuzo ya OBE aliyotunukiwa Katherine mwaka 2014 kwa mchango wake katika muziki na shughuli za hisani. Pia ilidaiwa alitoa kauli zilizomkera msanii huyo wa Wales.
Baadaye Katherine amesema hakuwahi kuombwa radhi na Beckham wala watu wake, ingawa alisisitiza kuwa hakutaka kuendelea kuishi na chuki na aliamua kuendelea na maisha yake.
Katika michuano ya Wimbledon mwaka huu, Beckham alionekana mwenye furaha akipiga picha za kumbukumbu akiwa na mama yake na kushuhudia mechi mbalimbali, huku Katherine naye akifurahia tukio hilo pamoja na mumewe na wageni wengine.
Ingawa hakuna aliyetoa kauli kuhusu kukutana kwao, picha zao zimesambaa kwenye mitandao ya kijamii na kuzua mjadala mkubwa, huku wengi wakitafsiri ukimya wao kuwa ishara kwamba tofauti zao bado hazijaisha licha ya kupita karibu muongo mmoja tangu sakata lao lianze.