Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

UCHAMBUZI: Suala la Amissi Tambwe litufunze mengi

HABARI kubwa iliyotamba na kujadiliwa sana wiki iliyopita ilikuwa ni suala la Yanga kuzuiwa na Shirikisho la Kimataifa la Soka (Fifa) kusajili kwa misimu mitatu mfululizo baada ya kushindwa kumlipa mshambuliaji wake wa zamani, Amissi Tambwe.

Tambwe anaidai Yanga Sh43.5 milioni, malipo ya mshahara wake na donge la usajili. Kwa mujibu wa taarifa, suala hilo liliamuliwa kwanza na Kitengo cha Usuluhishi wa Migogoro cha Fifa (DRC) na baadaye Yanga wakakata rufaa Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS), ambako pia walishindwa.

Ingawa Fifa ina tabia ya kufungia klabu kwa adhabu za vipindi vya usajili, yaani kipindi cha mwisho wa msimu na katikati ya msimu au dirisha dogo, taarifa ambazo zimekuwa zikitangazwa na pande zote zinasema wamefungiwa misimu mitatu.

Kwa maana hiyo, hawataweza kusajili katika vipindi sita, kama taarifa hiyo inazungumzia msimu, yaani mwisho wa msimu huu, katikati ya msimu unaoanza, mwisho wa msimu ujao, katikati ya msimu utakaofuata na kuendelea hadi misimu mitatu iishe, adhabu ambayo inaweza kuwa kubwa ya kwanza kwa klabu. Klabu nyingi duniani zimepata adhabu mithili ya hiyo ya Yanga, ingawa kwao zilihusu vipindi vya usajili na si msimu. Ya karibuni kabisa ilikuwa ya Chelsea kuzuiwa kusajili kwa vipindi vitatu Februari, 2019 na ikaanza adhabu kwa kutosajili kipindi cha joto, huku ikiwa imekata rufaa Mahakama ya Kimataifa ya Michezo (CAS).

Lakini adhabu hiyo ilipunguzwa Novemba mwaka huo baada ya CAS kukubaliana na hoja za vigogo hao wa England, lakini wakawapa onyo la kutorudia ukiukwaji wa kanuni za usajili wa wachezaji wadogo, pia kuipiga faini.

Barcelona walitumikia adhabu yao hadi ilipoisha, Real Madrid ikapunguziwa adhabu huku Roma ikizuiwa kusajili vipindi viwili vya usajili kwa kosa la kumsajili Phillipe Mexes wakati akiwa na mkataba na klabu Auxerre ya Ufaransa, adhabu ambayo pia ilipewa Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini kwa kumsajili Andriamirado ‘Dax’ Andrianarimanana wakati akiwa na mkataba nchini kwao Madagascar.

Suala la klabu hizo mbili za mwisho ni kama linalozungumzwa sasa la Bernard Morrison kusaini mkataba na Simba wakati Yanga inadai ilikuwa na mkataba halali ambao TFF iliamua kuchukua madaraka ya mahakama ya kuubatilisha. Kwa hiyo, Yanga haitakuwa timu ya kwanza kuzuiwa kusajili, ingawa kosa lake ni tofauti na ya klabu nilizozitaja hapo juu.

Lakini kuna baadhi ya mambo nimeona yanatoa somo kwa klabu zetu kutokana na adhabu hiyo hata kama Yanga itaipangua. Kwanza ni jinsi Yanga itakavyoweza kukabiliana na hali ya kutosajili kwa muda huo mrefu.

Klabu za Tanzania zina tabia ya mazingaombwe. Kusema zina vikosi vya vijana wakati hazina. Ukiulizia U-20 ya Yanga, utaambiwa ipo na ukiitaka utaletewa, hali kadhalika U-17. Lakini wanafanya mazoezi wapi, ni kitendawili.

Hawa ni wachezaji ambao huweza kuisaidia timu katika kipindi kigumu kama hicho. Wale wanaoonekana kuanza kukomaa ndio huanza kupewa nafasi, hasa ikitiliwa maanani lazima baadhi wataondoka mwisho wa msimu.

Pia mfumo wa klabu za Tanzania wa kuachana na wachezaji si mzuri. Mchezaji akionekana hajakomaa tu, anaachwa bila ya kufikiria angeweza kuisaidia timu hapo baadaye iwapo angetolewa kwa mkopo na kuwa anafuatiliwa kila hatua.

Wachezaji wanaotolewa kwa mkopo ili waende kupata nafasi katika vikosi vya kwanza vya klabu nyingine hurudishwa katika kipindi kama hicho na wakafanya vizuri. Yaani kama Yanga ingeachana vizuri na Yusuf Mhilu kwa kumtoa kwa mkopo kwenda Ndanda kabla ya kusajiliwa Kagera, lao ingekuwa inafikiria kumrejesha iwapo adhabu ya Fifa inasimama. Suala jingine ni kutokurupuka katika usajili. Klabu zetu huwa kama zinaamshwa usingizini usajili unapofika. Huwa hazina malengo ya muda mrefu na wachezaji zinaowataka.

Mfano wenzetu husajili wachezaji kwa malengo ya muda mrefu, yaani unamnunua leo na kumuacha aendelee kubakia klabu yake kwa msimu mmoja na baadaye kumchukua. Huyu pia aweza kuwa msaada wakati timu inapofungiwa kusajili kwa kuwa anakuwa ameshaingizwa katika vitabu.

Lakini kwa nini wachezaji wakimbilie Fifa wakati Shirikisho la Soka nchini (TFF) lina Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji inayoweza kushughulikia suala hilo na kulipatia ufumbuzi ambao utekelezaji wake ni nafuu?

Nakumbuka kuna wachezaji watatu ambao waliwasilisha malalamiko yao kuhusu malipo. Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ilishughulikia kesi zao na kuamuru walipwe madai yao. Klabu ziliposhindwa kuwalipa, kamati ikakazia hukumu na TFF ikatekeleza kwa kuzikata klabu hizo mapato yao ya mlangoni hadi madeni yalipoisha.

Tumeunda hivi vyombo ili vishughulikie kero za wachezaji na uwezo huo upo.

Ninavyojua, kamati ikishughulikia suala hilo hadi mwisho, hata mchezaji akienda Fifa, ni rahisi klabu kujitetea kwa kutumia mchakato wa ndani ambao Fifa wanauamini.

Ni bahati mbaya tu wakati fulani Yanga walizembe kuwasilisha ushahidi wa kumalizana na Njoroge kama kamati ilivyoamua na hivyo suala lake kuamuliwa kwa upande mmoja.

Kitu muhimu ni kamati hizi kuaminika na wadau wote ili mashauri yasikimbizwe Fifa, bali yajadiliwe na kuamuliwa humu ndani na kila upande ukaridhika.

Ingawa Fifa wanaamua, lakini wanabaki na maswali kwamba huko Tanzania kuna nini hadi suala la malipo ya mishahara na fedha za usajili lipelekwe kwao.

Hii haitoi taswira nzuri kwa muundo wetu wa utoaji haki. Ni lazima tujifunze katika kila tukio linalotokea.

Imeandikwa na ANGETILE OSIAH