Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Taifa Stars tiketi ipo Kwa Mkapa

Stars Pict
Stars Pict

Muktasari:

  • Ushindi wa bao 1-0 wa Guinea dhidi ya DR Congo umefanya kundi hilo kuwa gumu zaidi kwa nafasi moja iliyosalia 2025 katika hatua ya kufa au kupona, hasa kwa Taifa Stars. Kwa sasa, nafasi ya Stars kufuzu inategemea mchezo wa mwisho dhidi ya Guinea hapo kesho kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

TIKETI ya Tanzania kwenda fainali za Afcon 2025 ipo Kwa Mkapa. Ndio, ushindi wa mabao 2-0 ugenini dhidi Ethiopia, uliiweka Tanzania pazuri kabla ya Guinea kupata ushindi nyumbani mbele ya vinara wa kundi H, DR Congo iliyotaka tiketi mapema kabla ya mechi hizo za juzi usiku.

Ushindi wa bao 1-0 wa Guinea dhidi ya DR Congo umefanya kundi hilo kuwa gumu zaidi kwa nafasi moja iliyosalia 2025 katika hatua ya kufa au kupona, hasa kwa Taifa Stars. Kwa sasa, nafasi ya Stars kufuzu inategemea mchezo wa mwisho dhidi ya Guinea hapo kesho kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Guinea ina pointi tisa ikiwa nafasi ya pili, huku Stars ikishika nafasi ya tatu ikikusanya pointi saba, hivyo ushindi pekee ndio utakaowapeleka Watanzania kwenye fainali za AFCON kwa mara ya nne katika historia.

Kwa nini mchezo huu ni muhimu? Ni nafasi adimu kwa Tanzania kujihakikishia sehemu kwenye ramani ya soka la Afrika kwa mara nyingine. Mchezo huu si tu fursa ya kihistoria, bali pia kipimo cha uwezo wa Stars chini ya kocha Hemed Suleiman ‘Morocco’. Tutaangazia kile ambacho Stars inahitaji kufanya ili kushinda mchezo huu, changamoto zinazowakabili, na umuhimu wa sapoti ya mashabiki. 


ST05
ST05

MATUMAINI YALIVYOJENGWA 

Taifa Stars ilipata ushindi muhimu wa 2-0 dhidi ya Ethiopia katika mchezo wa awali uliochezwa Kinshasa, DR Congo. Ushindi huo ulionyesha uwezo wa Stars, hasa katika kipindi cha kwanza ambapo Simon Msuva na Feisal Salum walifunga mabao mawili muhimu. Ushindi huu uliwapa Watanzania matumaini na kuwaweka katika nafasi nzuri kabla ya mchezo wa mwisho. 

Katika mchezo huo, nafasi ya Novatus Dismas kwenye mfumo wa uchezaji wa Stars ilibainika kuwa muhimu hasa kwenye eneo la kiungo. Alisaidia kusambaza mipira kwa ufanisi, akihakikisha safu ya ushambuliaji inapata nafasi za wazi. Ustadi huu ulisaidia kufanikisha bao la Msuva katika dakika ya 15, ambalo lilitokana na mpira wa haraka wa kona ambao aliuchonga. 

Aidha, ushindi huu uliongeza morali ya wachezaji na mashabiki, huku kocha Morocco akiwapongeza kwa kujituma na kujitoa kwao. “Wameonyesha moyo wa kushinda. Ushindi huu ni hatua muhimu kuelekea kufanikisha ndoto ya Watanzania,”€  alisema kocha huyo. 

Kwa upande wa Ethiopia, kocha wao, Mesay Teferi alikiri udhaifu wa kikosi chake, akisema walishindwa kuhimili kasi ya Stars katika kipindi cha kwanza, lakini aliwapongeza wachezaji wake kwa kuonyesha juhudi kubwa hasa katika kipindi cha pili cha mchezo. 


ST04
ST04

GUINEA NA STARS

Guinea ni timu yenye uzoefu mkubwa na inajivunia wachezaji wanaocheza ligi za Ulaya, akiwemo mshambuliaji nyota Serhou Guirassy wa Borussia Dortmund. Bao lake dhidi ya DR Congo ambalo ni la sita ndani ya mechi tatu, limewapa Guinea nguvu ya kuingia katika mchezo wa Jumanne wakiwa na morali ya juu.

Stars inapaswa kujiandaa kwa changamoto ya kudhibiti kasi na ujuzi wa wachezaji wa Guinea, hasa Guirassy. 

Mojawapo ya changamoto kubwa kwa Stars itakuwa ni uwezo wa Guinea kutumia nafasi chache walizo nazo. Wanapokuwa katika presha, bado wanajua jinsi ya kuutuliza mchezo na kushambulia kwa haraka. Hii ina maana kwamba Stars wanapaswa kuwa makini kwa dakika zote 90 na kuepuka makosa madogo ambayo yanaweza kugharimu. 

Hata hivyo, faida ya kucheza nyumbani ni fursa kubwa kwa Stars. Uwanja wa Benjamin Mkapa umekuwa sehemu ya mafanikio kwa Stars, na mashabiki wao wamekuwa chachu ya ushindi katika mechi nyingi. Mashabiki wanapaswa kujitokeza kwa wingi na kuhamasisha wachezaji wao kwa kila dakika ya mchezo. 


ST03
ST03

MIKAKATI YA USHINDI

Kiungo cha Taifa Stars kina jukumu kubwa la kuhakikisha wanadhibiti mpira. Mudathir Yahya, Novatus Dismas, na Feisal Salum wanapaswa kucheza kwa ufanisi mkubwa, wakiunganisha safu ya ulinzi na ushambuliaji. Kudhibiti kasi ya mchezo kutawazuia Guinea kupata nafasi za kutawala mchezo. 

Stars inapaswa pia kutumia kasi ya Simon Msuva, Clement Mzize, na Mbwana Samatta kushambulia. Mipira ya krosi kutoka kwa mabeki wa pembeni kama Shomary Kapombe na Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ inaweza kuwa silaha madhubuti dhidi ya mabeki wa Guinea. Ushirikiano wa haraka na mipango kabambe ya ushambuliaji inaweza kuwa njia ya kupata mabao mapema. 

Safu ya ulinzi ya Stars, ikiongozwa na Dickson Job na Ibrahim Hamad, inapaswa kuwa makini sana dhidi ya washambuliaji wa Guinea. Wameonyesha uwezo wa kutumia nafasi ndogo kufanikisha mabao. Nidhamu ya juu na mawasiliano bora kati ya mabeki na kipa Aishi Manula ni muhimu. 

Mchezo huu unahitaji mshikamano wa timu nzima. Wachezaji wanapaswa kuwa na mawasiliano mazuri na kila mmoja kufahamu nafasi yake. Kukosekana kwa mpangilio kutatoa nafasi kwa Guinea kuchukua udhibiti wa mchezo. 


ST02
ST02

KUWA NYUMBANI

Presha za ushindi zinaweza kuwa changamoto kubwa kwa Stars. Wanacheza nyumbani, mbele ya mashabiki wao, na matarajio ni makubwa. Kocha Hemed Morocco anapaswa kuwasaidia wachezaji wake kudhibiti mawazo na kuingia uwanjani wakiwa na utulivu. 

Mashabiki nao wanapaswa kuwa chanzo cha motisha badala ya presha. Ni muhimu kuonyesha usaidizi mzuri kwa wachezaji hata wanapokumbana na changamoto uwanjani. 

Aidha, kocha Morocco anapaswa kusoma mchezo wa Guinea kwa kina. Kuweka mabadiliko ya mbinu yanayolingana na hali ya mchezo itakuwa muhimu kuhakikisha timu inabaki na nafasi ya kushinda hadi mwisho wa dakika 90.


ST01
ST01

FAINALI ZA NNE?

Taifa Stars kesho itakuwa na kazi moja ya kurudia ilichowahi kukifanya katika mihula mitatu tofauti iliyopita ilipokata tiketi ya kwenda fainali za Afcon.

Fainali za kwanza ilienda 1980 kwa kutaka tiketi ugenini kwa sare ya 1-1 dhidi ya Zambia baada ya awali kupata ushindi wa bao 1-0 nyumbani, shukrani kwa kiungo Mohammed Rishard ‘Adolph’ kabla ya Augustino Peter ‘Tino’ kufunga bao ugenini katika sare dhidi ya KK Elevens (sasa Chipolopolo).

Kisha ikaja mwaka 2019 tukakata tiketi tukiwa nyumbani kwa ushindi wa 3-0 dhidi ua Uganda iliyokuwa imefuzu mapema na fainali zilizofanyika mwaka huu, zilizokuwa za mwaka 2023 tulikata tiketi tukiwa ugenini dhidi ya Algeria kwa kutoka nao suluhu, huku wenyeji wakiwa wameshafuzu mapema na shukrani kwa Niger kuitibulia Uganda kwa kuifumua mabao 2-0.

Safari hii tunarudi nyumbani ili kwenda Morocco, tunahitaji ushindi pekee mbele ya Guinea kesho na hilo linawezekana kama Stars itaamua kukomaa mbele ya wageni jambo ambalo kila Mtanzania anahitaji, kwani tiketi ipo Kwa Mkapa.