Sure Boy , acha maisha yaendelee

MIONGONI mwa usajili bora uliowavutia mashabiki wa Yanga dirisha dogo msimu huu ni kusajiliwa kwa kiungo wa Azam, Salum Abubakar ‘Sure Boy’.

Kiungo huyo fundi amesajiliwa na Yanga baada ya majaribio mengi ya kutaka kumsajili kushindikana.

Mwanaspoti lilifanya mahojiano na Sure Boy aliyeanza kuonyesha cheche kwenye Kombe la Mapinduzi linaloendela kutimu vumbi Zanzibar akiwa na jezi ya Yanga.


MAISHA AZAM

Sure Boy ni miongoni mwa wachezaji walioupiga mwingi Azam kwa muda mrefu kwani alianza kuichezea 2007 hadi alipohamia Jangwani msimu huu.

Ki-ungo huyo anamtimu hiyo kumpatia kila kitu cha msingi katika maisha ya soka ndani na nje ya uwanja.

Anasema aliishi katika mazingira sahihi na mazuri akiwa na viongozi na wafanyakazi wa azam waliopita ndani ya klabu hiyo.

“Nimeamua kubadilisha mazingira kutoka Azam na kuja Yanga kutokana na changamoto mbalimbali ambazo zilikuwa nje ya uwezo wangu, hivyo nikaamua kufanya uamuzi mgumu,” anasema.

Sure Boy anasema alipanga kucheza muda mrefu zaidi katika kikosi cha Azam na kumalizia maisha ya soka hapo, lakini baadhi ya mambo yaliyotokea yamemfanya abadili uamuzi.

“Nilipanga kutoondoka kwenda katika timu yoyote na nimalizie soka langu Azam kwani kila ambacho nilikuwa nahitaji katika maisha yangu ya soka walinipatia tena kwa wakati sahihi,” anasema.

“Katika maisha kuna wakati unalazimika kufanya uamuzi mgumu ili mambo mengine yaende vizuri ndio kama ambavyo nimefanya, nimeamua kwenda kutafuta maisha mengine.”


KURUDI AZAM

Sure Boy anasema katika maisha hakuna kinachoshindikana, kama ambavyo alifanya uamuzi wa kuondoka Azam, basi moyo wake unatamani kuona anarejea katika timu hiyo siku moja.

Anasema uamuzi alioufanya haukuwa rahisi kwake ndio maana mpaka sasa haamini kama ameiacha Azam aliyoichezea kwa miaka 14.

“Ambacho naamini ni kwamba sijaondoka kwa ubaya Azam, bali ni sababu za maisha kwa hiyo kama itatokea nitahitajika kurudi tena nipo tayari,” anasema.


KUSIMAMISHWA

Kabla ya Sure Boy kujiunga na Yanga, mchezaji huyo alikuwa amesimamishwa na Azam pamoja na Mudathir Yahya na Aggrey Morris.

Baada ya muda Morris na Mudathir walikubali kurudi katika kikosi, lakini Sure Boy akaamua kutimkia Yanga.

“Kosa lilitokea katika vyumba vya kubadilishia nguo baada ya mechi na viongozi waliamua kutusimamisha baada ya tukio hilo ambalo nisingependa kuliongea kwa undani zaidi,” anasema.

“Jambo limeshapita na sitaki kusema zaidi kama mgawo wa pesa ndio ulikuwa tatizo ila tuliheshimu uamuzi wa viongozi kuamua kutusimamisha na sasa tuache maisha yaendelee. Azam ni timu ambayo imenilea na hivyo vyote ambavyo vimetokea ni vitu vya kawaida katika maisha.”


KUTIMIZA NDOTO

Sure Boy anasema kila m-che-zaji katika maisha ya soka ana ndoto anazopanga kutimiza, lakini hata siku moja hakuwa na ndoto za kucheza Yanga kwani alitaka kumalizia soka Azam.

“Kutoka ndani ya moyo wangu kabisa naongea ukweli, nilitamani kumalizia maisha yangu ya soka katika kikosi cha Azam kutokana na mambo makubwa waliyonifanyia, ila haya ya kuhama timu hii ndio yameshatokea hakuna jinsi,” alisema.

“Imetokea fursa nikaona acha nije kucheza Yanga kwa nguvu zangu zote ili kuweka alama kama ilivyokuwa Azam na kama nao watakubali na kuvutiwa zaidi na kazi yangu nitamalizia soka hapa.”


USHINDANI YANGA

Mashabiki wa soka nchini wanajiuliza Sure Boy anatacheza nafasi ya nani pale Yanga kwa jinsi kikosi hicho kilivyosheheni viungo mahiri msimu huu.

Katika eneo analocheza kuna wachezaji watano wenye ubora wanaocheza kikosi cha kwanza mara kwa mara ambao ni Khalid Aucho, Yanick Bangala na Feisal Salum wakati benchi kuna Mukoko Tonombe na Zawadi Mauya.

Sure Boy anasema haogopi ushindani wa namba na anaamini ataingia kikosi cha kwanza.

Anasema mpira ni uwanjani hivyo ataonyesha kiwango bora mazoezini na kumuachia Nasreddine Nabi aamue atamtumia wapi. “Ambacho naamini kama nikifanya mazoezi vizuri na kufuata kile ambacho kocha anahitaji, basi nitapewa nafasi ya kucheza mara kwa mara katika kikosi cha kwanza,” anasema.

“Naheshimu ubora wa kila mchezaji aliye katika kikosi cha Yanga. Wote wanastahili kuwepo hapa lakini na mini nimekuja kuongeza kitu ili kufikia mafanikio msimu huu.

“Yanga ni timu kubwa huwezi kusajiliwa hapa kama hauna ubora. Kama ambavyo wao waliniamini na kuona kitu kwangu, nitapambana kuipagania klabu hii ili kufikia kile ambacho kila mmoja anatamani kukiona kutoka kwangu.


SIKU YA KWANZA

Sure Boy anasema siku ya kwanza alipofika katika kambi ya Yanga iliyopo Kigamboni alipokewa vizuri na wachezaji, viongozi na benchi la ufundi. “Nimependa mazingira ya kambi yanavutia na imekuwa sehemu sahihi kwa wachezaji kukaa kwani hakuna vitu vingi na muda mwingi unafikiria kazi ya mpira tu.

“Nilipata nafasi ya kuongea na wachezaji ingawa si wote kama ilivyokuwa kwa benchi la ufundi niliongea na kocha nikaahidi kuwa tayari kufanya naye kazi kwa nguvu zote na kuifikisha Yanga katika mafanikio,” anasema.


ALAMA/ MAUMIVU

Sure Boy anasema katika maisha ya soka ndani Azam kitu kilichomuumiza zaidi ni kuondoka kwa nahodha, John Bocco.

“Kuondoka kwa Bocco ndani ya Azam niliumia sana na nilienda kuandika katika mitandao yangu ya kijamii kuonyesha hisia zangu kwa umma kuwa niliumia.

“Niliumia kwa sababu Bocco alikuwa ameitoa timu mbali na ameifanyia makubwa haikustahili kuwa vile,” anasema Sure Boy.