Simba si ya mchezo mchezo

Simba si ya mchezo mchezo

SIMBA kwa sasa inashika nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 35 katika mechi 15 ilizocheza.

Timu hii ina viporo vingi kwani imecheza mechi 15 ikifuatiwa na Namungo ambao wamecheza mechi 14 huku zingine zikiwa zimecheza 18 na zipo zenye michezo 17.

Mwanaspoti liliangalia rekodi za Simba katika mechi zake mpaka sasa kasi wanayokwenda nayo kwenye Ligi Kuu.

VINARA KUTUPIA

Simba ndio kinara kwa kutupia mabao katika Ligi Kuu hiyo baada ya kufunga mabao 37 mpaka sasa. Tayari wanaonyesha kwamba safu yao ya ushambuliaji iko vizuri katika mechi hizo imewazidi Yanga ambao wamecheza mechi 18 lakini wamefunga mabao 29.

Katika washambuliaji ambao wana mabao kuanzia matano, wamewatoa kina John Bocco ambaye ni kinara na mabao manane, Clatous Chama akiwa nayo sita na Meddie Kagere mabao saba.

Kwa safu hii ya ushambuliaji inaonyesha Simba wana uwezo wa kupata bao katika kila mechi kutokana na kasi ya ufungaji waliyonayo.

MECHI 10 HAWAJAFUNGWA

Wakiwa wamecheza mechi 15, Simba wamecheza 10 bila kupoteza huku wakitoka sare mbili na kupoteza mbili. Kutopoteza katika mechi 10 kunawafanya washike nafasi ya pili katika msimamo ambao msimu huu umekuwa na ushindani mkali. Vilevile wanashika rekodi ya kucheza raundi ya kwanza huku wakiwa hawajapoteza mechi nyingi kwani

Yanga inayoshika nafasi ya kwanza imeshinda mechi 13, hivyo Simba ni ya pili katika rekodi hiyo.

BAO NYINGI RAUNDI YA KWANZA

Licha ya kwamba kila timu imeshinda mechi zake nyingi, Simba wao wana rekodi yao msimu huu ya kufunga mabao mengi.

Rekodi kubwa ambayo wanaishikilia ni ya kuifunga Coastal 7-0 katika uwanja wa Mkwakwani, Tanga, huku idadi hiyo ikiwa haijafungwa na timu yoyote mpaka sasa. Idadi hiyo inaifanya pia Coastal kuweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza kuchapwa mabao mengi katika mechi moja kwenye mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Bara.

Simba pia katika raundi hii ushindi wao mkubwa mwingine ni wa mabao manne baada ya kuifunga Biashara 4-0, JKT TZ 4-0, Ihefu 4-0 na wa 5-0 dhidi ya Mwadui FC.

YEYOTE ANACHAPWA KWAO

Simba sio timu ambayo inategemea mshambuliaji mmoja inapokuwa uwanjani kwani kila mchezaji anafunga anapopata nafasi.

Simba mpaka sasa ina washambuliaji watatu machachari ambao wameonyesha kwamba hawana masihara katika kufunga baAda ya kila mmoja kuwa bora anapopata nafasi.

Bocco ana mabao nanane, Kagere akiwa na mabao saba, Chama anayo sita na Chris Mugalu anayo matano. Hali hii inawafanya hata wapinzani wao kutojua ni yupi sahihi wa kumkaba kwani kila mchezaji wa Simba kuanzia katika nafasi ya beki mpaka ushambuliaji anaweza kufunga muda wowote.

NYUMBANI, UGENINI WATAMU

Katika mechi ambazo Simba wamecheza katika mzunguko wa kwanza, wameonekana kuwa bora katika mechi za ugenini na nyumbani bila kuegemea upande mmoja.

Simba katika mechi zake za ugenini matokeo yao ni Ihefu 1-2 Simba, Mtibwa 1-1 Simba, JKT TZ 0-4 Simba, Yanga 1-1 Simba, Dodoma 0-4 Simba, Coastal 0-7 Simba na Mbeya City 0-1 Simba.

Katika mechi zao za nyumbani yako hivi; Simba 4-0 Biashara, Simba 0-1 Ruvu Shooting, Simba 5-0 Mwadui, Simba 2-0 Kagera Sugar, Simba 1-0 Kmc, Simba 2-0 Polisi Tz na Simba 4-0 Ihefu.