Real Madrid ingemsikiliza Ronaldo ingekuwa na kikosi hiki 2018
Muktasari:
- Bila shaka, CR7 aliishia kuondoka klabuni hapo mwaka 2018 baada ya kuhisi hakupata uungwaji mkono wa kutosha kutoka kwa rais wa klabu, Florentino Perez.
MADRID, HISPANIA: SUPASTAA Cristiano Ronaldo ni mmoja wa wachezaji bora zaidi katika historia ya Real Madrid na kama vigogo hao wa Hispania wangesikiliza ushauri wake mwaka 2018, basi wangekuwa na kikosi cha kutisha sana.
Bila shaka, CR7 aliishia kuondoka klabuni hapo mwaka 2018 baada ya kuhisi hakupata uungwaji mkono wa kutosha kutoka kwa rais wa klabu, Florentino Perez.
Kwa mujibu wa ripoti za wakati huo, Ronaldo alitaka Real Madrid wasajili wachezaji wachache maalum, na kama klabu ingefuata ushauri wake, hivi ndivyo wangejipanga msimu wa 2018/19 kwa kuwa na sura hizi katika kikosi chao.
Kipa: David De Gea
Hatimaye Real Madrid ilimsajili Thibaut Courtois, lakini Ronaldo alikuwa anasisitiza zaidi kusajiliwa kwa David De Gea.
Ingawa hakuna ubishi kiwango cha kipa huyo wa Kihispania kilishuka mwishoni mwa muda wake Manchester United, mwaka 2018 bado alihesabiwa kuwa mmoja wa makipa bora duniani. Kwa kweli, kama si kwa tatizo la mashine ya kutuma faksi mwaka 2015, huenda tayari angekuwa mchezaji wa Real Madrid.
Beki wa kulia: Dani Carvajal
Ronaldo alicheza mechi 165 pamoja na Carvajal akiwa Real Madrid, huku beki huyo wa kulia akimpatia Ronaldo pasi za mwisho 13 katika kipindi hicho.
Kwa kuwa hakusukuma kusajiliwa kwa beki mwingine wa kulia wakati huo, inaonyesha kuwa Ronaldo alikuwa ameridhika na Carvajal katika nafasi hiyo.
Beki wa kati: Marquinhos
Hata hivyo, CR7 alikuwa na hamu kubwa ya kuona mabadiliko makubwa katika safu ya ulinzi baada ya klabu kushindwa kuweka rekodi nzuri ya kutofungwa mara kwa mara msimu wa 2017/18. Mara kadhaa iliripotiwa Ronaldo alitaka klabu imsajili Marquinhos, lakini hawakufanikiwa kumng’oa kutoka PSG.
Beki wa kati: David Alaba
Miaka mitatu kabla Alaba hajajiunga rasmi na Real Madrid, Ronaldo aliripotiwa kuomba asajiliwe.
Nyota huyo wa zamani wa Bayern Munich alikuwa mmoja wa mabeki bora zaidi duniani wakati wa ubora wake, akiwa na uwezo wa kucheza kama beki wa kati au beki wa kushoto.
Mashabiki wa Real Madrid hatimaye walimwona akijiunga na klabu mwaka 2021 kwa uhamisho wa bure, lakini kwa misimu ya hivi karibuni amekuwa akipambana zaidi na majeraha.
Beki wa kushoto: Marcelo
Kwa kuzingatia Ronaldo alitaka Marcelo ajiunge naye Juventus, inaeleweka angempenda Mbrazili huyo aendelee kubaki Madrid kama asingetimka klabuni mwaka 2018.
Wawili hao walikuwa na maelewano ya ajabu upande wa kushoto, wakichangia jumla ya mabao 33 pamoja walipokuwa Madrid.
Kiungo mkabaji: Casemiro
Ronaldo na Casemiro daima wameonekana kuwa na uhusiano mzuri.
Walikutana tena Manchester United mwaka 2022, na kwa mujibu wa ripoti, CR7 baadaye alijaribu kumshawishi Mbrazili huyo ajiunge naye Al-Nassr.
Mwaka 2018, Casemiro huenda alikuwa kiungo bora zaidi wa ulinzi duniani.
Kiungo wa kati: Toni Kroos
Kroos alikuwa kiungo kilichoishikilia Real Madrid pamoja, na si ajabu kwamba safu ya kiungo imeonekana kuyumba zaidi tangu astaafu mwaka 2024.
Mwaka 2018, alikuwa mmoja wa majina ya kwanza kabisa kwenye kikosi cha kwanza na kwa haki kabisa.
Kiungo wa kati: Luka Modric
Ingawa Ronaldo alitaka mabadiliko makubwa mwaka 2018, alikuwa tayari kabisa kuacha kiungo wa kati kama kilivyo.
Inaonekana hakuwahi kupendekeza klabu isajili kiungo wa kati mpya, jambo linaloashiria kuwa alikuwa ameridhika na chaguo za kiungo zilizokuwepo wakati huo. Na hata sasa, Modric bado anang’ara.
Winga wa kulia: Gareth Bale
Baada ya kufunga mabao mawili akiwa mchezaji aliyetokea benchini kwenye fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya 2018, Bale bila shaka angekuwa sehemu ya mipango ya Ronaldo kwa siku zijazo. Staa huyo wa Wales aliendelea kucheza mara kwa mara msimu wa 2018/19, lakini alianza kupoteza nafasi msimu uliofuata. Hata hivyo, Bale alikuwa mchezaji muhimu sana kwa Madrid, hata mwishoni mwa kipindi chake.
Straika: Cristiano Ronaldo
Kufikia wakati huo, Ronaldo alikuwa ameanza kucheza zaidi kama mshambuliaji wa kati sambamba na Karim Benzema, badala ya winga.
Kama CR7 asingegombana na Perez, kuna uwezekano mkubwa angekuwa mshambuliaji wa kwanza wa Madrid msimu wa 2018/19, huku Benzema akiondoka klabuni. Isitoshe, msimu wa 2017/18, Benzema alikuwa ametoka kwenye msimu wake mbaya zaidi wa ufungaji akiwa Madrid, akifunga mabao matano tu ya ligi katika mechi 32.
Winga wa kushoto: Neymar
Mwaka 2018, Real Madrid walikuwa wakihusishwa sana na Neymar, ambaye alisemekana kuwa na kutoridhika PSG wakati huo.
Alipoulizwa kama Mbrazili huyo angeweza kucheza pamoja na Ronaldo Madrid, Marcelo alisema: “Kwa nini Neymar asiweze kuja na Cristiano abakie? Chumba cha kubadilishia nguo kinamtaka Cristiano abaki. Na milango ya Real Madrid iko wazi daima kwa Neymar. Madrid lazima daima iwatafute wachezaji bora. Siku moja Neymar atachezea Real Madrid.”
Kwa bahati mbaya, dili hilo halikuwahi kutimia, na Neymar aliishia kucheza PSG kwa miaka mitano iliyofuata.