ATM YA WIKI: Nadal amestaafu na pesa zake

Muktasari:
- Staa huyu anastaafu akiwa amepata mafanikio ya kutosha kwa kushinda jumla ya mataji 103 katika kipindi chote alichohudumu na leo tutaungazia utajiri ambao ameupata kupitia mchezo huo na madili mengine.
MAJORCA, HISPANIA: MWEZI huu ulikuwa ni mwisho kwa mchezaji wa tenis raia wa Hispania. Rafael Nadal kucheza mchezo huo, baada ya kutangaza kustaafu akiwa na umri wa miaka 38.
Staa huyu anastaafu akiwa amepata mafanikio ya kutosha kwa kushinda jumla ya mataji 103 katika kipindi chote alichohudumu na leo tutaungazia utajiri ambao ameupata kupitia mchezo huo na madili mengine.
ANAPIGAJE PESA?
Tangu aanze rasmi kucheza tenis kama mchezaji wa kulipwa, Nadal amekunja jumla ya Dola 134 milioni katika mashindano yanayojumuisha mchezaji mmoja kuanzia mwaka 2001.
Anashika nafasi yapili katika orodha ya wachezaji wa tenis waliokunja mpunga mrefu zaidi katika mashindano ya aina hiyo nyuma ya Novak Djokovic.
Nadal pia anapiga pesa kupitia ubalozi wa kampuni ya utengenezaji wa magari ya Korea Kusini, Kia, ambayo amesaini nayo mkataba tangu mwaka 2006.
Kampuni nyingine anayofanya nayo kazi ni Nike iliyokuwa ikimtengeneza mavazi na viatu alivyokuwa anatumia katika mashindano mbalimbali.
Pia ni balozi wa kampuni ya utengenezaji wa biskuti na mikate kutoka Hispania iitwayo Quely, ambayo amekuwa anafanya nayo kazi tangu mwaka 2010.
Wadhamini wengine muhimu wa Nadal ni pamoja na Santander, Emporio Armani, Babolat, Heliocare, Telefonica, Banco Sabadell, Tommy Hilfiger, Mapfre, Insure na Go.
Ameweka pia katika tenis amefungua akademi yake mwenyewe iitwayo ‘Rafa Nadal Academy’ huko Manacor, Majorca, Hispania.
Ndani ya akademi hiyo kuna kituo cha mazoezi chenye madarasa mbalimbali yanayotolewa kwa watoto wanaojiunga na programu hiyo, viwanja vya kuchezea tenis na vifaa vyengine muhimu kwa ajili ya kufundishia watoto. Hapa amekuwa akijipatia pesa kupitia wadhamini na ada zinazolipwa na watoto anaotaka kujifunza.
Nadal pia alishirikiana na mwimbaji Enrique Iglesias na baadaye nyota wa soka Christian Ronaldo kuwekeza kwenye migahawa ya Kihispania ya TATEL.
Mgahawa wa kwanza ulifunguliwa huko Madrid, ukifuatiwa na mingine huko Ibiza na Miami.

NYUMBA
Kwa mujibu wa ripoti, Nadal anamiliki nyumba kadhaa ikiwamo huko Mallorca, Hispania yenye thamani ya Dola 1.5 milioni, na jumba la kifahari katika Jamhuri ya Dominika, alilonunua kwa Dola 2 milioni lililoko Porto Cristo nchini humo.

NDINGA
Ferrari 458 Italia-Dola 314,000
Aston Martin DBS-Dola 314,000
Mercedes-Benz AMG GT-S-Dola 175,900
Mercedes-Benz SL55-Dola 112,850
Kia EV6 GT-Dola 61,600.
Kia Stinger-Dola 54,065

MSAADA KWA JAMII
Nadal alianzisha taasisi yake ya ‘Rafa Nadal Foundation’ mwaka 2008 huko Hispania baada ya kushinda taji lake la nne la French Open.
Taasisi hii imejikita katika kusaidia watoto yatima na vijana kwa jumla.
Katika kuishi hilo, taasisi hii ilisaidia kuanzishwa kwa Kituo cha Elimu cha Anantapur kwa ajili ya kusomesha watoto yatima na wale wa mitaani.
Mbali ya kutoa misaada kupitia taasisi yake, Nadal pia ameshiriki katika kampeni kadhaa, mechi za hisani kwa ajili ya kuchangisha pesa za kusaidia jamii.

MAISHA NA BATA
Yupo kwenye ndoa na mrembo Maria Francisca tangu mwaka 2019 na Oktoba 2022 walifanikiwa kupata mtoto wao wa kiume ambaye ndio wakwanza kwao.