JAMVI LA KISPOTI: Julio ametujibu kwa vitendo,wengine wajitathimini

JAMVI LA KISPOTI: Julio ametujibu kwa vitendo,wengine wajitathimini

Hatua kubwa ya mafanikio kwa soka la nchi wiki hii ni kuibuka kidedea ka kikosi cha timu ya vijana chini ya umri wa miaka 20 Ngorongoro Heroes kutinga hatua ya fainali ya mashindano ya Ukanda wa Afrika Mashariki na kupoteza kwa kufungwa mabao 4-1 dhidi ya Uganda.

Ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Sudan Kusini ni hatua inawafanya kukata tiketi moja kwa moja kutinga Fainali za Mataifa Afrika kwa vijana wa umri huo yatakayofanyika mwakani Februari 14 nchini Mauritania.

Hii inakuwa ni fursa ya kwanza kwa timu za vijana kushiriki fainali hizo za Afcon.

Jambo zuri zaidi ni kwamba safari hii makocha wa timu hiyo wote ni wazawa wakiiwezesha timu hiyo kukata tiketi hiyo muhimu pengine hata kuzidi kombe la Cecafa na kikois hicho kikionyesha kandanda zuri la ushindani .

Timu hiyo ipo chini ya kocha mwenye hulka ya kuongea sana Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ akisaidiana na wenzake kina Idd Abubakar kuipeleka timu hiyo katika fainali kubwa zaidi za soka ikiwa ni hatua ya mafanikio mengine.

Julio amekuwa akilia kwa muda mrefu kwamba amekuwa akidharauliwa na kukumbukwa pale tu mambo yanapokuwa magumu akipewa timu za klabu na hata zile za taifa na sasa amejibu kwa vitendo kwa kuipa nchi heshima hiyo.

Alichofanya Julio ni kuthubutu kuonyesha kile anachoweza katika taaluma yake ya ukocha na sio kitu kigeni kuona anafanikiwa kwa kuwa miaka ya nyuma alikuwa mchezaji muhimu kwa taifa na sasa akiwa kama kocha.

Julio ni binadamu hulka yake ya kuongea sana isiwe kigezo cha kudharaulika kwasasa anahitaji heshima yake na athaminiwe ikiwezekana kuendelezwa kwani anaweza kuja kuwa hata Kim Poulsen wetu na kulisaidia zaidi taifa.

Ajira ya ukocha nayo inahitaji kujiendeleza shida ya makocha wengi wetu hawataki kujiendeleza kulinganisha na mataifa mengine ambayo yamekuwa yakizalisha makocha wengi ambao wanakuja hata kuvuna pesa nyingi hapa kwetu na kuendeleza nchi zao.

Mfano mzuri tuangalie wingi wa makocha kutoka Burundi wanavyoendelea kujaa nchini wakitawala katika klabu zetu na hata sasa timu za taifa,ifike wakati shirikisho na hata serikali kuliona hili kwa jicho pana na kuamua kuweka utaratibu wa kuwaendeleza makocha wetu wa ndani.

Fursa kama hii pia inahitaji utayari wa makocha hao kuchangamka na kuzikimbilia kwani wapo makocha wanakimbia elimu hizi na kuitaka kuendelea kuishi maisha ya mazoea ya kukariri badala ya kuwa na elimu ya kisasa.

Soka linazidi kupiga hatua na kwenda katika teknonolojia zaidi katika mazingira hayo hutamani kuona tena kuna makocha wanakimbia elimu hizi au kukimbilia wakati wakiambiwa ni lazima wakasome na wsipofanya hivyo hawataweza kufanya kazi zao.

Hili ndio eneo ambalo makocha wengi wa kigeni wanawaacha wazawa wetu na kubaki nyuma kisha baadaye tunakuwa wazuri wa kulalamika,inawezekaan wao kupata fursa za kupata mafanikio kama wataona umuhimu wa kubadilisha mitazamo yao na kuachana na mazoea.

Tumekuwa tukishuhudia makocha wakubwa duniani Pep Guardiola, Jose Mourinho, Jürgen Klopp na wengine wengi wakikutana katika mafunzo mbalimbali ya soka katika kujiweka kisasa zaidi kwa kuwqa zama zinabadilika kadiri ya muda unavyosogea.

Wakati Fulani huko nyuma aliyewahi kuwa kocha wa Yanga Mholanzi Ernie Brandts alilazimika kuiacha timu hiyo kwa siku chache akirudi kwao Ulaya kuhudhuria mafunzo ya ukocha na ndani yake alikuwa darasa moja na Guardiola.

Brandts hakusubiri kualikwa aliona fursa ya mafunzo hayo na kuomba kisha kulipa fedha na baadaye kwenda kushiriki,nidhamu hii inatakiwa kufanywa kwa vitendo na makocha wetu wa ndani ili nao waweze kushika nafasi kama hizo na kulipa taifa mafanikio.