Z Anto kuwaimbia 'live' Binti Kiziwi warembo na watanashati viziwi

Muktasari:

Mkali wa kibao cha 'Binti Kiziwi' Z Anto anatatajia kuwa mmoja wa wasanii watakaotoa burudani kesho katika mashindano ya kumsaka mrembo na mtanashati kiziwi Afrika.

Mkali wa kibao cha 'Binti Kiziwi' Z Anto anatarajia kuwa mmoja wa wasanii watakaotoa burudani kesho katika mashindano ya kumsaka mrembo na mtanashati kiziwi Afrika.

Hayo yamesemwa leo Alhamisi Septemba 30, 2021 na Katibu wa Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dk Hassan Abbasialipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mashindano hayo.

Mashindano ya Mr na Miss Viziwi, yanafanyika Afrika na kwa mara ya kwanza Tanzania itakuwa mwenyeji.

Dk Abbasi amesema katika mashindano hayo ambayo yatafanyika ukumbi wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam kuanzia saa moja jioni, wasanii mbalimbali wataburudisha akiwemo Z Anto aliyevuma na kibao cha 'Binti Kiziwi'.

"Kesho Z Anto atawaambia live 'Biinti kiziwi' wenzetu hawa wenye uziwi na kutakuwa na mkalimani atakayewatafsiria maana ya wimbo huo, kwani nao kama binadamu wengine wana haki ya kupenda na kupendwa pia," amesema Katibu huyo.

Wasanii wengine watakaokuwepo amewataja kuwa ni Sholo Mwamba ambaye atautambulisha muziki wa Singeli Afrika na msanii wa nyimbo za asili na sarakasi, One Star.

Wakati kuhusu maandalizi ya mashindano hayo,amesema yamefikia pazuri na tayari washiriki kutoka nchi 12 Afrika wameshawasilibna wanaendelea na mazoezi.

Aidha ameeleza kuwa wanatarajia watu zaidi ya 600 kushiriki kuona mashindano hayo,wakiwemo wageni waalikwa,mabalozi,wasanii mbalimbali huku kiingilio kwa atakayefika kesho kikiwa Sh10,000.

Warembo nawatanashati 60 wanatarajiwa kupanda jukwaani kuchuana huku Tanzania ikiwakilishwa na warembo wanne na watanashati wanne.