Paula afanya jambo, akwepa kumzungumzia Rayvanny

Paula Paul ambaye ni mtoto wa msanii Kajala Masanja anatarajia kufungua duka lake la nguo alilodai limegharimu Sh500 milioni.
Hilo limebainika leo Julai 3, 2022, alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha The Switch kwenye kituo televisheni cha Wasafi.
Licha ya kutotaka kuweka wazi ni nini anchokwenda kukifanya siku ya Ijumaa, lakini baba yake muziki Paul Matthysse ’P.Funk’, aliwahi kuiambia mwananchi kuwa mtoto wake huyo anatarajia kufungua duka lake la nguo maeneo ya Sinza.
“Paula sasa amekuwa na anafikiria kufanya mambo makubwa na kwa kuwa anapenda sana mambo ya mavazi,  ana mpango pia wa kufungua duka lake la nguo siku za karibuni, nadhani atawaambia,” alisema Majani.
Akizungumza  leo, Paula alisema ana jambo kubwa analokwenda kulifanya siku ya Ijumaa na alipobanwa kwamba limemgharimu Shilingi  ngapi alijibu kuwa ni Sh500 milioni.
Kwa majibu hayo ni wazi kuwa Paula duka hilo ndilo litakuwa limemgharimu Sh500 milioni na sio kingine.
Alipoulizwa amepata wapi fedha za kufungua mradi huo, alijibu kuwa zimetokana na matangazo mbalimbali ambayo amekuwa akiyapata.


AZUNGUMZIA MATUMIZI YAKE

Paula amesema mama yake humpa Sh1 milioni kwa ajili ya matumizi.
Alijikuta akilisema hilo baada ya kuulizwa na mtangazaji kuwa baada ya kufikisha miaka 20 nini anaona kimebadilika kwake.
"Naweza sema nimeacha utoto, kwani zamani mama alikuwa akinipa Sh1 milioni za matumizi naweza kwenda kufanya shopping, lakini sasa hivi huwa nawaza kuifanyia mambo mengine ya kimaendeleo,” amesema Paula
Pamoja na mambo mengine, Paula aliulizwa kuhusiana kinachoendelea kuhusu mahusiano yake na msanii wa Bongo Fleva, Raymond Mwakyusa ’Rayvanny’ ambapo anaelezwa wameachana.
Katika hilo,Paula  amesema asingependa kuliongelea jambo hilo.