Msanii na mshehereshaji Zipompa afariki

MSANII na mshehereshaji maarufu nchini, Gladys Chiduo ‘MC Zipompa’ amefariki dunia.
Taarifa za kifo chake zimethibitishwa leo Jumanne Novemba 10,2020 na mlezi wa Chama cha Washehereshaji nchini Tanzania(SAA), Cynthia Henjewele.
Akizungumza na Mwanaspoti Online, Cynthia amesema Zipompa ambaye alijizolea umaarufu kupitia uigizaji, amefariki saa 9 usiku wa kuamkia leo Jumanne akiwa anapelekwa hospitali.
“Zipompa enzi za uhai wake alikuwa akisumbuliwa na presha,  ambapo juzi (Jumapili Novemba 8, 2020) hali yake haikuwa nzuri na kwenda hospitali ya Masana iliyopo Tegeta ambapo alilazwa hapo na kuruhusiwa jana (Jumatatu) asubuhi.
“Hata hivyo ilipofika jana saa 9 usiku akiwa nyumbani kwake Mbweni hali yake ilibadilika, na tulipowasiliana watu wake wa karibu na kwenda kumchukua kwa ajili ya kumpeleka hospitali ndio hivyo tena kumbe alikuwa amefariki tangu tunatoka nyumbani,” ameeleza mlezi huyo wa SAA.
Amesema pamoja na msiba huo kutokea muda mrefu walishindwa kutoa taarifa kutokana na watoto wake wote kuwa nje ya nchi.
Hivyo walichofanya ni kushirikiana kwanza na ndugu zao na kupata kibali cha kufanya hivyo mchana huu ambapo watoto hao tayari wameanza safari ya kuja nchini wakitokea Marekani.
Msiba upo nyumbani kwake Mbweni ambapo mipango ya ratiba za mazishi  inaendelea.
Cythia amesema watamkumbuka mshehereshaji huyo kwa mengi, ikiwemo ucheshi wake na ushirikiano na watu.
Cythia amesema watamkumbuka mshehereshaji huyo kwa mengi, ikwemo ucheshi wake na ushirikiano na watu.