Luiza Mbutu: Kukata uno kuheshimiwe
Muktasari:
- Kipande kile kiliwapendeza watu wengi hasa wapenda muziki wa dansi, hadi wengine wakasema Luiza bado anang’ara kwenye kukata mauno ikiwa ni kazi ambayo alianza nayo kabla ya kuingia kwenye kuimba.
HIVI karibuni kulikuwa na kipande cha video kilichokuwa kinatembea kwenye mitandao ya kijamii kilichomhusu kiongozi na mwimbaji mkongwe wa bendi ya ‘Twanga Pepeta’ Luiza Mbutu, akiwa stejini akikata mauno.
Kipande kile kiliwapendeza watu wengi hasa wapenda muziki wa dansi, hadi wengine wakasema Luiza bado anang’ara kwenye kukata mauno ikiwa ni kazi ambayo alianza nayo kabla ya kuingia kwenye kuimba.
Lakini Luiza ameeleza jinsi anavyosumbuliwa na wanaume kutokana na uchezaji wake akiwa stejini na kutaka kazi hiyo iheshimiwe kama kazi zingine.
Mwimbaji huyo ambaye ni mtunzi wa wimbo maarufu wa ‘Kuolewa’ kutoka Twanga Pepeta kwenye Albamu ya Fainali Uzeeni, alisema licha ya kupata usumbufu huo, lakini amekuwa akijitunza na kujiheshimu kwani anafanya hivyo kulinda kazi yake na heshima yake kama mwanamke.
“Unajua watu wakisikia Luiza Mbutu, basi wanajua ni kati ya wamoja ya wanawake ambao hawajiheshimu, na waelewe mimi ninaposimama stejini pale nakuwa kazini na kitu nachozingatia sana ni kuilinda kazi yangu, hivyo wanapotokea wanaume wenye tamaa ya mahusiano mimi nachokifanya siku zote ni kuwa mbali nao kabisa ndiyo maana nashinda vishawishi hivyo kila siku,” alisema Luiza.
Mwimbaji huyo ni mmoja kati ya wasanii wa kike ambao wanatumia viuno kuwapagawisha mashabiki wake akiwa stejini, na ni muimba mzuri mwenye sauti ya kipekee.