Kwa Mobetto bado hakujaeleweka

Unakumbumba Jumapili iliyopita wakati sakata la video za Rayvanny akipigana mabusu na mtoto wa muigizaji Kajala Masanja, Paula kusambaa na Kajala kuibuka na kudai kuwa aliyemkuwadia binti yake kwa Rayvanny ni mwanamitindo Hamisa Mobetto?

Sasa baada ya tuhuma zile Hamisa kupitia mwanasheria wake walimpa Kajala saa 12 tu kufuta tuhuma hizo na kuomba radhi vinginevyo wangemshughulikia kisheria, lakini Kajala hakufuata maelekezo hayo. Gazeti hili lilimtafuta mwanasheria wa Hamisa, Elia Rioba na kutaka kujua mchakato wao umeendeleaje ikiwa sasa imeshatimia wiki moja tangu wampe maelekezo Kajala, ni hatua gani wameshachukua ambapo amefunguka wameamua taarifa za mchakato huo zibaki kuwa za ndani. “Kwa sasa tumeamua taarifa za mchakato huu zibaki ndani, kama kuna jambo lolote ambalo vyombo vya habari mtatakiwa kujua tutawajulisha,” alisema Rioba.

Hata hivyo, inaonekana ni kama upande wa Hamisa umeamua kupotezea suala hilo tangu Hamisa pamoja na Rayvanny walipoitwa kituo cha polisi Osterbay kwa ajili ya mahojiano.