Kilichompeleka Munalove kwa Zari ni hiki

NDANI ya wiki mbili, mjasiriamali Muna Love, ameonekana katika picha na video akiwa na watoto wa Zari aliozaa na Diamond.

Watoto hao ni Latifa na Nillan, ambao mtandaoni wana wafuasi kibao kuwashinda hata mastaa wengine wakubwa Bongo.

Wakati Latifa akiwa na wafuasi milioni 2.7, Nillan ana wafuasi milioni 1.1.

Muna Love ambaye jina lake halisi ni Rose Alphonce, ameonekana akiwa na watoto hao huku picha zao zikiwa zinarushiwa kwenye kurasa zao hizo.

Jambo hilo lilifanya Mwanaspoti kumtafuta Muna kujua kulikoni kugandana na watoto hao wa staa namba moja Bongo kwa sasa, Diamond Platnumz.

Katika maelezo yake Muna ambaye aliwahi kueleza gazeti hili kwamba huwa akiwavalisha nguo watoto hao, kazi aliyoianza miaka miwili iliyopita, alisema kilichompeleka ni kazi hiyohiyo.

Hata hivyo, tofauti na zamani ambapo alikuwa akizituma kwa usafiri wa anga (ndege), hivi sasa Zari amemtaka aende ili akawasimamie watoto hao kuwavalisha wakati wa kupigwa picha mbalimbali.

Muna alisema amekwenda na mabegi makubwa mawili yaliyojaa nguo ambazo zote amepatiwa mkwanja wa zaidi ya Sh11 milioni.

“Kwangu hii ni faraja kubwa sana kupata dili kama hili ukizingatia Zari ni mtu maarufu na anafuatiliwa na watu wengi.

“Kupitia kazi aliyonipa ameweza kuniunganisha na watu wengine kufanya nao kazi na ninaona nikipiga hatua nyingine katika biashara yangu hiyo ya nguo za watoto,” alisema Muna.


MKATABA WAO

Muna ambaye pia ni msanii wa maigizo, anasema waliingia makubaliano hayo mwishoni mwa mwaka 2019, akiwa nchini China ambako alipigiwa simu na Zari kumpa oda ya nguo za Nillan.

“Nikamtumia nilizonazo achague anazozipenda kisha akanitumia pesa nami nikamtumia mzigo na ndio kuanzia hapo akanipa oda kila mwisho wa mwezi nimtumie nguo,” anasema

Kuhusu bei ya nguo zake anasema inategemea, ambapo za kawaida ni Sh65,000 na brandi za majina makubwa huanzia Sh100,000 hadi Sh500,000.