Gigy Money afungiwa miezi sita

Muktasari:

Sambamba na adhabu ya kufungiwa  pia ametakiwa kulipa faini ya Sh1 milioni, adhabu ambayo imetolewa kwa mujibu wa kanuni za Baraza hilo za mwaka 2018.

Baraza la Sanaa la Taifa (Basata), limemfungia miezi sita msanii wa Bongo Fleva nchini Tanzania, Gift Stanford maarufu Gigy Money, kutojihusisha na sanaa ndani na nje ya nchi.

Taarifa iliyotolewa leo Jumanne Januari 5, 2021 na Kaimu Katibu Mtendaji wa Basata, Matiko Mniko, ilisema Gigy akiwa katika tamasha la Wasafi ‘Tumewasha Tour’ lililofanyika jijini Dodoma katika uwanja wa Jamhuri , alipanda jukwaani kwa ajili ya kutumbuiza na kuvua gauni (dela) na kubakia na vazi ambalo lilikuwa linaonyesha maungo yake ya mwili.
Sambamba na adhabu ya kufungiwa pia ametakiwa kulipa faini ya Sh1 milioni kwa kosa hilo, adhabu ambayo imetolewa kwa mujibu wa kanuni za Baraza hilo za mwaka 2018.
“Kitendo alichokifanya Gigy,  kilionyesha maungo yake ya mwili na hivyo kuudhalilisha utu wake na kubughudhi hadhira ya wapenda sanaa ndani na nje ya nchi.
“Alikifanya huku akifahamu kuwa tukio linalorushwa mubashara na televisheni ya Wasafi na kuonwa na watu wa rika  mbalimbali na hivyo kwenda kinyume na kanuni za Baraza za mwaka 2018.
“Kutokana na ukiukwaji wa sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa shughuli za sanaa nchini, Baraza limemfungia kujihusisha na shuguli za sanaa kwa kipindi cha miezi sita ndani na nchi ya nchi,|”.
Hata hivyo Matiko ,amesema, Baraza limeridhishwa kuwa alikiuka maadili ya kazi za sanaa kwenye Tamasha husika na kikiuka kifungu 4(L) cha Sheria namba 23 ya mwaka 1984 (Re:2002), Kanuni 25 (6)(9) ya kanuni za Baraza za mwaka GNN.43/2018 na taratibu za uendeshaji wa shughuli za sanaa nchini,”alisema Katibu huyo.
Taarifa hiyo pia ilieleza kuwa msanii huyo alishaitwa mbele ya Baraza na kuonywa mara kadhaa kwa vitendo vya ukiukwaji wa maadili na kuahidi kutorudia tena.
Pia alitumia fursa hiyo kuwakumbusha wasanii wote nchini kufanya shughuli za sanaa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu.