Koffi, Cindy na Nandy ndani ya Kivuruge remix
Muktasari:
- Machi, 2020 mwanamuziki wa Jamhuri ya Kidemokrasia Congo (DRC), Koffi Olomide alipokuja Tanzania alieleza namna anavyomfuatilia msanii Nandy na kukiri kuupenda wimbo wa Kivuruge wa msanii huyo.
Dar es Salaam. Wakati remix ya wimbo Kivuruge wa msanii Nandy aliomshirikisha Koffi Olomide na Cindy ikisubiriwa kwa hamu, ni kama mashabiki wameonjeshwa hivi utamu wa wimbo huo.
Jana Jumamosi Februari katika shoo ya Koffi iliyopewa jina mahaba ya rhumba iliyofanyika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam, mwanamuziki huyo aliyeshirikishwa na Diamond Platnumz katika wimbo wa Waah, alimpandisha Nandy jukwaani na kuimba pamoja remix ya wimbo huo wakiwa sambamba na msanii Cindy aliyekuja nchini na Koffi.
Juzi wakati Nandy akizindua wimbo wa Leoleo alieleza mipango ya kuufanyia remix wimbo huo na kumshirikisha Koffi.
Wakati Nandy akipanda jukwaani wengi walijua ataimba wimbo wa Leoleo, badala yake wakaimba remix ya Kivuruge.
Koffi alimtambulisha Nandy kwa Cindy na kuwataka wasalimiane na kisha kuimba wimbo pamoja.