Siri ya Mzee Pembe kufanikiwa vichekesho

Muktasari:

Kama kuna kitu hakipendi mzee Pembe kwa wasanii wanaochipukia katika vichekesho ni kiki zinazodhalilisha sanaa hiyo.

MSANII mkongwe wa vichekesho nchini, Mzee Pembe amesema licha ya ongezeko la chipukizi wengi katika tasnia hiyo,baadhi hawafuati maadili ya kazi.
Amesema sekta ya vichekesho haihitaji kiki kama ilivyo nyingine, kutokana na uigizaji wake wakuwapa furaha watu baada ya kuchoshwa na masumbuko ya  ulimwengu.
Bali kinachotakiwa anashauri wachekeshaji nchi wawe wanaangalia hali halisi ya vitu ambavyo vipo katika jamii waelimishe kwa njia ya kuchekesha.
"Vichekesho ni tiba ya magonjwa ya moyo,leo unapodanganya ukweli ukawa mwingine kesho basi inakuwa ngumu kesho kukuamini.
"Nawashauri vijana licha ya teknolojia kukua lazima wajitahidi kuwa wabunifu,pia waepukane na kiki ambazo zinakuwa zinachafua tasnia, naamini kazi ikiwa nzuri watu wataiamini na kuipenda," amesema Mzee Pembe.
Mbali na hilo amezungumzia kwa upande wa kazi zake kwamba bado anaendelea kuzifanya akishirikiana na Senga.
"Tunaangalia upepo wa ugonjwa wa covid 19, ukipita salama tutaanza kwenda mikoa mbalimbali kwa ajili ya shoo,ila sasa tunafanya tunavyorusha katika mitandao yetu ya kijamii,"amesema Pembe.