Ndoa yamtesa Gloria Muliro

Muktasari:

Kitu hicho mpaka leo kinamtesa Gloria, hakuamini ndoa yake ingefikia hatua hiyo lakini hakuwa na jinsi kuendelea nayo mambo yalipozidi.

ZIKIWA imepita miaka mitano tangu aombe talaka, msanii wa injili kichuna, Gloria Muliro bado anajutia kusambaratika kwa ndoa yake.

Gloria ambaye amekuwa kimya kwenye muziki kwa miaka miwili baada ya kurudi shuleni kusomea masuala ya dini, alifunga ndoa na aliyekuwa mume wake Pasta Mcongo Erick Omba Aprili 2010.

Ndoa hiyo ilidumu kwa miaka mitano na kufikia Januari 2015, ikavunjika. Kipindi hicho Omba alikuwa sio mume tu wa Gloria bali pia meneja wake.

Ni enzi ambazo Muliro alikuwa akitambaa kimuziki hivyo kuingia hela haikuwa ishu kwake. Na kutokana na kuwa alimwamini sana meneja wake, akawa amempa mamlaka ya kukusanya kipato chake kwa niaba yake. Hapo ndipo Omba akabadilika na kudaiwa kumchepukia Gloria na hata kumvunja. Mwisho wa siku kichuna huyo alichoka na kuamua kujitoa.

Kitu hicho mpaka leo kinamtesa Gloria, hakuamini ndoa yake ingefikia hatua hiyo lakini hakuwa na jinsi kuendelea nayo mambo yalipozidi.

“Hakuna mtu yeyote ambaye afungapo ndoa, hutamani ije kuvunjika. Hakuna. Hamna anayependa talaka. Binfasi sikudhani ingetokea na ilipokuja, ilikuwa ni moja kati ya bahati mbaya nilizowahi kupata. Sikupendelea ifikie hatua ya kuomba talaka lakini nikawa sina jinsi. Ndio hayo ni maisha na lazima nizidi kuishi.”