Mzee Yussuf arudi rasmi kwenye taarabu

Muktasari:

Mzee Yussuf alitangaza kuacha kuimba taarabu mwaka 2016 na kujikita katika shughuli za ualimu wa dini.

Unakumbuka Machi 12, 2020 Mzee Yussuf alipowashtua wengi pale alipoandika kwenye ukurasa wake wa Instagram kuwa anarudi mjini na ataimba mpaka agalegale.

Jambo hilo halikuwashtua tu mashabiki bali na baadhi ya viongozi wa dini kutokana na msanii huyo kuamua kujikita katika masuala ya dini.

Pamoja na kuhojiwa mara kwa mara kuhusu kauli hiyo hakuwahi kusema kuwa anarudi kwa staili gani hadi leo Jumatano Julai 22, 2020 kuweka tangazo katika ukurasa wake wa Instagram na kueleza tukio la uwepo wake katika viwanja vya Dar Live, tukio aliloliita 'Mzee Yussuf anarudi Mjini'.

Katika tangazo hilo alieleza pia wasanii wa taarabu watakaomsindikiza kuwa ni pamoja na mke wake Leyla Rashid, dada yake Hadija Yussuf.

Mwisho wa tangazo hilo aliweka maneno yaliyosomeka " Mungu pekee mwenye mamlaka na mimi na atanibariki Amin"

Wengine ni Fatma Mcharuko, Prince Amigo na mtoto Pori wote wakiwa ni waimba taarabu.

Kupitia tangazo hilo ni wazi kwamba sasa Mzee Yussuf aliyewahi kutamba na nyimbo mbalimbali zikiwemo “Mpenzi Chocolate”, “Daktari wa mapenzi”, “Nitadumu Naye” na “VIP” anaweza kuja na sapraizi kwa mashabiki zake.