Mimi Mars aingia 18 za Diamond

BAADA ya Tanasha Dona, nani atafuata kwenye listi ya pendapenda Diamond? Ndilo swali ambalo wapenda ubuyu wengi wanajiuliza. Huku baadhi yao wakijaribu kutengeneza majibu kwamba labda ni Zuchu, majibu ambayo mpaka sasa bado hayajapata uthibitisho.

Lakini mwishoni mwa wiki, Diamond ameweka wazi kumzimikia mwimbaji Mimi Mars ambaye ni dada wa damu wa mwanamuziki wa kike wa kimataifa kutoka Tanzania, Vanessa Mdee.

Kupitia akaunti yake ya Instagram Diamond aliposti video ikimuonyesha Mimi Mars akiimba wimbo wa Cheche wa Zuchu ft Diamond kisha chini akaandika maelezo ya kuchokoza jambo yanayosema: “Mi nakapendaga haka katoto… Sema sijui ata timing naikoseaga wapi Mwana wa Dangote… Doh!” Kisha akamalizia na kumtag Mimi Mars mwenyewe.

Hata hivyo, licha kutagiwa kwenye posti hiyo, Mimi Mars hakuja kuangusha maelezo yoyote wala kusema jambo kwenye akaunti yake. Inawezekana Diamond aliandika kwa masihara tu, lakini swali ni je kwanini masihara hayo alichagua kuyafanya kwa Mimi Mars tu, ikiwa kuna mastaa wengine wa kike pia waliposti video kama hiyo wakiimba.