Kuipata huduma kliniki ya Ronaldo ujipange aisee

Muktasari:

  • Kliniki hiyo iliyo kwenye mjengo wa kisasa wa ghorofa sita ina wataalamu wa nywele 150, wanaolipwa mshahara mkubwa na CR7.

KWA mteja yeyote atakayetaka huduma kwenye kliniki ya ubandikaji nywele yake Cristiano Ronaldo inayosimamiwa na demu wake Georgina Rodriguez, basi atahitaji kuwa na mkwanja wa maana.

Cristiano alifungua kliniki hiyo ya kisasa jijini Madrid, Machi 18 mwaka huu huku Rodriguez akiwa ndio bosi wa zaidi ya wafanyikazi 150 pale.

Kwa yeyote anayetembelea hospitali hiyo kubandikwa nywele au kurekebishiwa tatizo la nywele, anahitajika kulipia angalau Sh450,000. Kiasi hicho ndicho cha gharama ya chini kabisa kwa kutegemea na mahitaji ya mteja.

Kliniki hiyo iliyo kwenye mjengo wa kisasa wa ghorofa sita ina wataalamu wa nywele 150, wanaolipwa mshahara mkubwa na CR7.

Tayari CR7 kalipia Euro 1 milioni kwa mradi huo huku akitarajiwa kuongeza Euro25 milioni zaidi katika kipindi cha miaka mitatu au minne ijayo.