Kamanda Mambosasa ashindwa kuthibisha kujisalimisha kwa Idris Sultan polisi

Muktasari:

Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alimtaka Sultan kujisalimisha kituo chochote cha polisi baada ya kuweka picha yenye sura yake akiwa ameketi katika kiti chenye nembo ya Taifa.

Dar es Salaam. Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa ameshindwa kuthibitisha kujisalimisha mshindi wa Big Brother Africa 2014 na msanii wa vichekesho Idris Sultan licha ya kukiri kupata maagizo ya kutakiwa polisi.

Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alimtaka Sultan kujisalimisha kituo chochote cha polisi baada ya kuweka picha yenye sura yake akiwa ameketi katika kiti chenye nembo ya Taifa.

Pia, Idrisa aliweka picha nyingine inayoonyesha sura ya Rais John Magufuli akiwa amesimama huku amevaa suruali yenye mikanda inayoshikizwa mabehani (Suspenda).

Kamanda Mambosasa alisema kwa ufupi, “Nipo kituo kikuu cha polisi Dar es Salaam, lakini taarifa za kujisalimisha kwake huyo Idrisa Sultani kituoni hapa bado hazijanifikia, subiri nifuatilie.”

Awali Kamanda wa Polisi wa mkoa wa kipolisi wa Kinondoni, Mussa Taibu amesema hana taarifa kuhusu kujisamilisha kituo cha polisi Oysterbay.

“Inawezekana amejisalimisha nilipokuwa nje ya ofisi kwenye majukumu mengine. Ninazo taarifa za amri ya kujisalimisha kwa msanii huyo kwenye kituo chochote cha polisi jijini Dar es Salaam,” alisema na kuongeza.

“Mtu yeyote anapohusishwa na jambo lenye utata, tunalazimika kumhoji ili kuelewa mhusika alikuwa na maana gani. Tunafuatilia kujua amejisalimisha kituo gani cha polisi na ikitolekea hajafanya hivyo tutamtafuta na kumkamata.”