H Baba: Harmonize amenirudisha kwenye game

Muktasari:

Msanii wa muziki wa kizazi kipya Hamis Ramadhani 'H,Baba' ameweka wazi mwanamuziki mwenzake Rajabu Abdul Kahali  'Hamornize' amemrudisha kwenye 'game' kabla ya mwenyewe kuamua.

MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Hamis Ramadhani 'H.Baba'  amesema mkali wa Bongo Fleva, Rajabu Abdul Kahali 'Hamornize' ndiye amemrudisha kwenye 'game' kabla ya maamuzi yake na ameahidi si muda mrefu ataachia kitu cha maana.

H.Baba amesema toka mwaka 2015, alipumzika muziki na kujikita kwenye familia yake akilea watoto huku akijiandaa na majukumu mengine mapya. Kabla hajaanza harakati za kurudi kwenye muziki, Hamornize ameshamrudisha kupitia wimbo wake wa Uno. Ni baada ya kumtaja H.Baba akimsifia kwa mauno aliyokuwa anawadatisha mashabiki wake.

"Mimi nilikuwa kimya toka mwaka 2015, niliamua kulea kwanza wanangu halafu mambo mengine yafate, nilijipangia miaka mitano ipite ndio nirudi katika muziki. Sasa miaka mitano imeisha namshukuru Mungu. Sasa hata sijaamua kuanza harakati kurudi tayari watu wamenirudisha. Umeona kwa mwanamuziki Hamornize na wimbo wake wa Uno, kila mtu alikuwa 'attention' kuniona mimi katika kipengele hicho alichoniimba"

Aidha, H. Baba amesema pamoja na kujipanga kurudi kwake kurudi kwenye muziki, haoifii mabadiliko anayoyaona kwa wenzake na amesisitiza kati ya hao wote hakuna aliyeweza kuziba pengo lake katika kipindi chote alichokaa kimya na amewaomba mashabiki wake wasubiri kupata burudani siku si nyingi.