DNA ya nini? Mastaa wanaofanana na watoto zao ile mbaya

Wakati Hamisa Mobetto anatambulisha wimbo wake mpya aliomshirikisha Singh wa Nigeria, mtangazaji wa redio aliyokuwa anatambulisha wimbo huo alimuuliza kuhusu tetesi za kwamba mzazi mwenzake, Diamond Platnumz aliwahi kuwa na wasiwasi kwamba yeye sio baba halisi wa mtoto wao, Dylan hivyo ilibidi waende wakapime DNA — Hamisa akathibitisha kwamba jambo hilo ni kweli.

Akaongeza kwamba: “Tulienda hospitali, tukapima na baada ya wiki kama mbili tatu hivi majibu yakaja na mtoto akaonakena ni wake kwa asimili zote.”

Kwa kawaida wanaume wengi huwa na wasiwasi kuhusu ukweli wa nani baba wa mtoto pale tu inapotokea kuwa mtoto hafanani na mzazi huyo wa kiume. Sasa wakati upande mmoja wa shilingi kuna mastaa wana wasiwasi na watoto wao mpaka kufikia hatua ya kuhitaji DNA (sio kitu kibaya kupima DNA), upande mwingine kuna wasanii ambao wenyewe wana amani kwa sababu kwao walipiga ‘fotokopi’. Yaani watoto waliopata wanafanana nao mpaka unajiuliza DNA ya nini? Listi ya wasanii hao hii hapa.

Mwana-FA

MwanaFA ana watoto wawili wa kike, wa kwanza anaitwa Maleeka na mzuwanda wake mwenye miaka miwili. Ukiwaona watoto hao hasa huyo wa pili wala huhitaji kupewa mchambuzi akusaidie kuelewa kuwa ni mtoto wa damu ya Mwanafalsafa.

Kuanzia rangi nyeupe ya ngozi, midomo yenye rangi ya pinki, mpangilio wa meno kinywani mpaka mwanya - yaani watoto wamechukua kila kitu kama kilivyo kutoka kwa dingi yao. Septemba, mwaka jana, MwanaFA aliposti picha Instagram akiwa na watoto wake kwenye gari, kilichotokea baada ya hapo ilikuwa ni mfululizo wa comment za masihara kutoka kwa mastaa wenzake wakiomba mbinu aliyoitumia kupata watoto anaofanana nao kiasi hicho, kwa mfano Elizabeth Micheal ‘Lulu’ aliandika: “Nyinyi ni mapacha watatu.”

Alikiba

Kwenye suala la kufanikisha jukumu tulilotumwa na Mungu la kuijaza dunia, Kiba sio ‘mediocre’, ana watoto wanne mpaka sasa na wote amezaa na wanawake wanne tofauti. Yupo Amiya, Chammy, Sameer na Keyaan.

Hata hivyo kwenye upande wa kupiga ‘kopi’, Kiba anafanana zaidi na watoto wake wa kiume kuliko wa kike, ingawa kwa kutazama hata hao mabinti zake pia sura zao hazijaenda mbali sana. Kwa mfano ukitazama sura ya mtoto wake wa kwanza wa kiume ambaye ni wa tatu kwa Alikiba, Sameer Kiba ni kama unamtazama baba mtu. Wakati pia mtoto wake wa mwisho Keyaan ambaye amezaa na Amina Khaleef mrembo kutoka Mombasa Kenya, ni ‘copy and paste’ ya Alikiba mwenyewe.

Kwenye akaunti ya Instagram ya Keyaan kuna picha moja Keyaan ametokea amenyoosha kimdomo - ukitazama hiyo picha unaweza kusema ni King Kiba anasema ‘Yooo’ kabla ya kuanza kuimba.

Vicent Kigosi ‘Ray’

Usiombe Ray aposti picha ya mtoto wake anayeitwa Jaden huko Instagram halafu aje Wema Sepetu ku-comment. Utakuta kaandika ‘Jamani katoto kazuri mpaka natamani kukala’.

Sasa inavyoonekana ni kama staa huyu wa Bongo Movie alikuwa na script ya jinsi gani anataka afanane na mtoto wake, kwa sababu ukionyeshwa picha ya Jaden kisha ukapewa ya baba yake, wala huhitaji lulufu wa kukutafisria kuwa hao ni mtu na mtoto wake — wamefanana kinoma.

Pia kama hiyo haitoshi, kwa mbali dogo anafanana na mama yake muigizaji Chuchu Hans, ingawa bado anafanana zaidi na baba yake.

Single Mtambalike

Mtoto mkubwa wa muigizaji Single Mtambalike ndiye aliyemuingiza baba yake kwenye listI hii. Kwanza dogo anafanana na baba yake ile mbaya, na kama hiyo haitoshi, kwa sababu dogo ni mkubwa sasa, ana takriban miaka 24, ameanza kuota ndevu na kuna wakati huzinyoa kwa mtindo wa O kama baba yake.

Hata mtoto wake wa pili ambaye ni wa kike pia anafanana Single lakini sio kuzidi huyu wa kwanza. Na kuna uwezekano jamaa ana damu kali kiasi kwamba anafikia hatua mpaka ya kufanana na watoto wa waigizaji wenzake — kwa mfano, kuna kipindi alikuwa akifananishwa na mtoto wa muigizaji Steve Nyerere.

Diamond

Kwanza unaweza ukasema Diamond hafanani sana na watoto wake, hapo utakuwa umeangalia picha ya watoto wake Tiffa, Nilan na Dylan. Lakini ukitazama picha ya mtoto wake wa mwisho Naseeb Junior wanafanana ile ile.

Hata hivyo, mwanzo mtoto huyo alikuwa anafananishwa na muigizaji Mwijaku, lakini kadri siku zinavyozidi kwenda, dogo anazidi kukua na kuchukua sura ya mzee wake na hilo linaonekana kwa urahisi zaidi picha zao, yaani ya Diaomond na mtoto wake zikipostiwa pamoja. Zaidi wanachofanana ni sura zao za duara, midomo yao yenye lips nene, pua na mikato ya nyusi zao pia.