Mtibwa yalazimishwa sare Simba

Muktasari:

  • Mtibwa ni bingwa wa Ligi Kuu Bara mara mbili ilitwaa taji hilo 1999 na 2000

Dar es Salaam. Kipa wa Mtibwa Sugar, Benedict Tinoco amesema hakupata misukosuko mikubwa walipocheza na Simba, ila amempa sifa Emmanuel Okwi kuwa ni mshambuliaji anayejua anachokifanya uwanjani.

Okwi alifungia Simba bao la kusawazisha katika dakika 90 kwa mpira wa adhabu uliokwenda moja kwa moja wavuni na kuisaidia Simba kupata sare ya bao 1-1 na Mtibwa Sugar jana kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Akizungumza na tovuti ya www.mwanaspoti.co.tz kipa Tinoco alisema anasifu Okwi siyo kwa sababu amenifunga bao la mpira wa adhabu, ila alikuwa makini pale mbele, laiti kama angepata mtu sahihi anayemwelewa anataka nini ningekuwa na wakati mgumu, ila tunashukuru Mungu, tunaangalia mechi ya mbele.

Tinoco alisema Okwi anautumia vema uzoefu wake hata kama timu inazidiwa anajua jinsi ya kuwatuliza wachezaji wenzake na kucheza kwa akili kuhakikisha wanapata matokeo.

"Hatuibezi Simba ina wachezaji wazuri, kila timu kwetu tunaona ina ushindani tunapoingia uwanjani tunaingia na akili ya kwenda kupambana na siyo kuona tuna haki ya kupata matokeo kirahisi," alisema kipa huyo.

Amewazungumzia mastaa waliyotoka Mtibwa Sugar na wanacheza Simba, kwamba wana viwango vya juu na siyo wa kuwabeza huku akisema kujuana muda mrefu kuliwafanya washindwe kufurukuta katika mchezo huo.

"Tunawajua vizuri wanatujua vizuri, hilo lilitupa wakati mgumu sana pande zote mbili kujua nini kifanyike ili kupunguza kasi ya kutamba uwanjani," alisema Tinoco.