Wema Sepetu naye yamkuta mahakamani

Muktasari:

Wema, ambaye ni Miss Tanzania mwaka 2006, anakabiliwa na shitaka hilo pamoja na wafanyakazi wake wawili.

MALKIA wa Bongo Movie, Wema Sepetu ameingia hatiani kwa kuonekana ana kesi ya kujibu katika mashitaka yake ya kutumia dawa za kulevya inayomkabili kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Wema, ambaye ni Miss Tanzania mwaka 2006, anakabiliwa na shitaka hilo pamoja na wafanyakazi wake wawili.

Uamuzi huo umetolewa jana na Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba na kwamba Wema na wenzake wataanza kujitetea Mei 14 na 15, mwaka huu.

Hakimu Simba alitoa uamuzi huo baada ya kupitia ushahidi uliotolewa mahakamani hapo na mashahidi watano wa upande wa mashtaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Constantine Kakula.

Kabla ya uamuzi huo kutolewa na Hakimu Simba, Wakili Kakula aliiambia mahakama kuwa jana kesi hiyo ilipangwa kwa ajili ya uamuzi kama washtakiwa hao watakuwa na kesi ya kujibu ama la ili waachiwe huru kwa mujibu wa hoja zilizowasilishwa kujitosheleza kwamba, washtakiwa wote wana kesi ya kujibu.

Wema na wenzake Angelina Msigwa na Matrida Seleman Abbas wanatetewa na Wakili Alberto Msando.