NO AGENDA: Penzi moto la mshua mengi kwa k-lynn limeukamata mtandao aisee!

DINGILAI Reginald Mengi ana mabovu ya kutosha tangu miaka ya 1970. Alianza kumiliki vyombo vya habari tangu mwanzoni mwa miaka ya 1990. The Guardian na magezeti yake. ITV na Radio One. East Africa TV na Radio. Ongeza na vingine.

Usiongee kuhusu viwanda kwa mshua Mengi. Ubia wake na Coca Cola siyo stori. Kwa sasa anakaribia kutuuzia simu made in Tanzania. Hata hivyo, kinachomfanya abambe sio hiyo mitikasi yake ya kupiga hela. Dingi ameushika mtandao kwa namna malovee yake yanavyoshika chati.

Yes, mshua aliamua kuwekeza moyo wake kwa mrembo ghali sana, Jacqueline Ntuyabaliwe ‘K-Lynn’. Dingalai mpaka amekuwa multi billionaire, maana yake anajua kucheza na fursa.

Alipomsogeza K-Lynn akaona isiwe tabu. Akamuoa mazima ili fursa isipotee. Jina official la K-Lynn kwa sasa ni Jacqueline Mengi!

K-Lynn ni staa tangu mwaka 2000 aliposhinda taji la Miss Tanzania. Baada ya hapo akatusua kwenye Bongo Fleva. Unakumbuka ngoma ‘Chochote Utapata’ ambayo alimshirikisha Noorah a.k.a Baba Styles? Vipi ‘Nipe Mkono’ alioingia booth na Mr Blue? Je, ‘Crazy Over You’ na Squeezer? Unaisahauje ‘Nalia Kwa Furaha’ aliyompa shavu Bushoke? Najua unaipata ‘Nikipata Wangu’ ambayo remix alipigwa tafu na Jay Mo. Halafu kuna Besti.

Kinachomfanya K-Lynn kubamba sasa siyo urembo wake wala haihusiani na muziki. Ananyoosha kwa penzi lake na mshua Mengi. Mabibi na mabwana, ubao unavyosomeka, Mengi ndiye sultan na K-Lynn ni sultana wetu bila kupepesa macho.

Wanasema mkwanja ndiyo umemlegeza K-Lynn kwa mshua. Kwani hatari kitu gani? K-Lynn ni kati ya warembo walioumbwa kwa utamu wa hali ya juu. Mpaka leo ukimuona ni baby face. Umbo na sura yake vinasadifu uhodari wa Maulana katika uumbaji. Kuna ubaya gani mshua kutuliza majeshi hapo? Inadhuru nini mrembo kujituliza palipo na ukwasi?

Kwani K-Lynn hajawahi kuwa na majanki? Jimmy Kabwe waliishia wapi? Kinjekitile wa Kingunge, alioa mwanamke mwingine wakati K-Lynn ndiye alikuwa mchumba wake wa miaka na miaka. Tusikumbushane stori ya Mzungu, K-Lynn na Miss Tanzania 2002, Angela Damas, walipotekwa wakidanganywa ni dili la mitindo kumbe mkasa wa mapenzi. K-Lynn amepitia mengi kama lilivyo jina la mista wake.

Halafu wanaume majanki utawaweza somo? Yaani mtoto mzuri kama K-Lynn akiwa na janki majanga. Janki atataka mrembo ampe hela badala ya yeye amhudumie. Mjini kuna warembo wanalazimika kuuza mapenzi kwa vibabu ili wapate hela za kuwapa majanki wao. Acha K-Lynn atulie na mshua.

NI COUPLE YA KITAIFA

Sema nini? Ukiidurusu public domain tangu mwaka 2011 mpaka 2018, imekuwa miaka saba ya supastaa Diamond Platnumz kuutawala mtandao kwa picha zake akiwa na wapenzi wake. Kama ilivyo hulka yake ya bandika bandua.

Diamond alishafunika mbaya na Wema Sepetu, aling’arisha na Penny, akanyoosha sana na Zari, juzi juzi mapichapicha na Tanasha yalikong’oli kunako internet domain. Ile mipicha ilifanya wadada wamuone Dangote ni gentleman malaika. Wakasema: Diamond anajua kucare!

Si unajua Diamond na shoo zake? Mara kabeba gauni la Wema lisiburuze chini mrembo akitembea. Halafu anaonekana anamvalisha viatu Tanasha. Anamfungulia mlango wa gari Zari. Very protective young man kwa akina mamsapu wake. Na haya ndo mambo wanawake wanapenda. Wanapenda kuonekana malkia. Shoo za Dangote kwa wapenzi wake zilifanya wadada wamtolee mfano kuwa mwanaume bora kimapenzi. Habari za Dangote kubadili wapanzi mara kwa mara hazikuwakera. Wao walisuuzika kumoyo na ule ugentleman wake wa kwenye kamera.

Nilimsikia ndugu yangu mmoja anashushuliwa na mkewe: “Hivi wewe yule mtoto mdogo Diamond anakushinda nini? Humuoni anavyomfanyia Zari, mpaka mwanamke unajiona malkia. Hutaki na mimi nijione malkia?” Dah! Dogo wa Tandale alileta mushkeli ndani ya familia za watu.

Siku hizi unadhani Dangote ana nyimbo basi? Tena baada ya kumnanga Mobeto kuwa ni mchawi, wanamwogooopaa! Wanawake hawapendi wanaume wenye kudhalilisha wanawake. Couple ya moto mjini ni mshua Mengi na K-Lynn.

Mtandao wameushika aisee! Mapichapicha ya mahabati. Siku hizi wanaume tunaambiwa: “Hamna hela na mahaba hamjui. Mengi ana pesa na mahaba anayajua.” Kimsingi mshua Mengi na K-Lynn ndiyo wanafunika mjini, ila kwetu pangu pakavu tabu ipo palepale. Wanaume tunahimizwa tuwe na hela, halafu tutoe good times kwa akina mamsapu kama mshua kwa K-Lynn.

Ukipitia twiti za mshua kwa K-lynn, namna anavyompamba, lazima uone donge! Mshua anajua kubembeleza na kumfanya mwanamke ajione malkia. Mara mshua aseme K-Lynn ndiyo pumzi yake, au amtamke ndiye dunia yake. Halafu anayesema hivyo ni mtu mwenye hela zake. Mtaani majanki hawana hela lakini hawaishi maringo kwa wanawake. Ebo! Acha mshua anyooshe!

Hii tabia ya majanki kuondoka njia kuu ya kiume, inayotaka wao ndiyo wawe walinzi wa wanawake wao, na kujipa sifa za kudeka, kulelewa na wakati huohuo siyo waamifu, ni sababu ya washua kama Prof Juma Kapuya kuchukua pointi nyingi kwa warembo wadogo na kuoa kiulaini, kisha mabishoo wanapigwa vibuti.

NAONA WANAFANANA

Kuna wakati nilikuwa nabisha kuwa wapendanao wakiishi muda mrefu huanza kufanana. Ukitazama picha za mshua Mengi na K-Lynn, naona sasa hivi wanafanana. Yaani wanarandana na wanashabihiana. Mwonekano wao saresare. Wanapendeza.

Mtindo mpya wa ndevu wa mshua unamwonesha ni Don. K-Lynn pia siyo yule wa Bongo Fleva na akina Blue, yupo tofauti na aliyekuwa kwenye line ya Miss Tanzania kwa Anko Lundenga. K-Lynn wa sasa ni mwanamke wa kishua. Anazungumza kishua. Na amesema kwa mshua hajafuata pesa bali mapenzi.

K-Lynn anavyowaza leo, si sawa na yule aliyekuwa analilia promo ya ngoma zake kwa ma-DJ ili apate shoo, aungeunge vijisenti. K-Lynn wa sasa anawaza mambo makubwa. Kuna vitu havimpi shida K-Lynn kuviwaza. Maana ni mama wa moja ya familia tano nchini, zilizobarikiwa uchumi mkubwa.

Halafu kinachovutia mshua ana mambo ya kisasa. Anajiweka kileo ili kwenda sawa mtoto wa kileo. Washua wengine mizinguo, anaoa mtoto mbichi halafu anataka mrembo ndiyo azeeke ili waende sawa, badala ya yeye kujiweka kwenye njia ya mkewe. Mshua Mengi yupo kwenye njia ya K-Lynn. Anamuona ni janki mwenzie.

Ushauri kwa wazee wenzangu; Tukitaka tujikute majanki ndoa na majanki lazima zihusike. Halafu mambo yanaonekana dhahiri kuwa ndoa na majanki ukiziweza na kuchomoza nazo vizuri, kuna uwezekano zinaongeza mpaka siku za kuishi. Tukubali, ndoa ya mshua Mengi na K-Lynn ndiyo couple ya kitaifa kwa sasa. Makofi kwao tafadhali.