CR7 sasa anaoa, mkewe huyu hapa

Muktasari:

Mama huyo, Dolores Aveiro alizungumzia maisha ya mapenzi ya mtoto wake pamoja na watoto wake wanne huku akimtaja mrembo Georgina Rodriguez kuwa anampenda sana.

LISBON, URENO. MAMA mzazi wa Cristiano Ronaldo sasa amefichua mwanaye huyo hana muda mrefu ataoa na tayari ameshapata mke wa kufunga naye pingu za maisha baada ya kupitapita kwa wanawake kibao wa aina tofautitofauti.

Mama huyo, Dolores Aveiro alizungumzia maisha ya mapenzi ya mtoto wake pamoja na watoto wake wanne huku akimtaja mrembo Georgina Rodriguez kuwa anampenda sana.

Ronaldo kabla ya hapo alikuwa kwenye penzi la Mwanamitindo wa Kirusi, Irina Shayk, lakini kwa mujibu wa mama yake, Dolores, mwanamke ambaye anamkubali ni Georgina.

“Ni mama wa mjukuu wangu. Mkwe wangu mtarajiwa. Bado hajawa mkwe wangu rasmi, lakini ni mtarajiwa. Ni mtu mtaratibu sana,” alisema mama yake CR7.

Mama huyo alipoulizwa kama anadhani mwanaye anahitaji kuwa na mtu wa karibu yake, alisema:

“Ndiyo. Tunafanya mambo mengi sana ya kijinga katika maisha, hivyo kuna nyakati unahitaji kuziacha hizo na kutengeneza maisha. Amefikia kwenye hatua hiyo.”

Dolores alisema alishtuka mara ya kwanza alipoambiwa kwamba amekuwa bibi kwa mtoto ambaye hakumfahamu mama yake na hivyo yeye ndiyo akafanya majukumu ya kuwa mama, wakati alipozaliwa mtoto wa kwanza wa Ronaldo, Cristiano Jr aka Cristianinho.