Madrid yamalizana na Hazard, yaisubiri Chelsea

Muktasari:

  • Winga wa klabu ya Chelsea na timu ya taifa Ubelgiji Eden Hazard uwezekano wa kubakia ndani ya timu hiyo unazidi kuwa finyu huku Real Madrid ikiongeza nguvu ya kumnasa staa huyo.

Inasemekana staa wa Chelsea, Eden Hazard amekubaliana maslahi binafsi na Real Madrid hivyo inajiandaa kuanzisha mazungumzo na Chelsea huku ikitazamiwa kuweka mezani dau la Pauni 150 milioni kukamilisha uhamisho wake katika dirisha kubwa lijalo la majira ya joto.

Madrid inataka kumtumia staa wake, Mateo Kovacic anayekipiga kwa mkopo Chelsea kama chambo wa kukamilisha uhamisho huo na inamuona Hazard kama mchezaji ambaye atapunguza maumivu ya pengo la Cristiano Ronaldo.

Mkataba wa Hazard na Chelsea unatazamiwa kumalizika mwishoni mwa msimu ujao na Chelsea haitazamiwi kupanga dau kubwa kwa staa huyo na endapo atakuwa hajasaini mkataba mpya mpaka kufikia mwishoni mwa msimu huu itafungua mlango wa kuondoka.