Kucheza samba mnashindwa, mnataka nini tena...!

Karibuni tena kwenye jamvi la Anti K, kama kawaida huwa tunakutana hapa siku ya Jumapili kupeana mawili matatu yahusuyo masuala ya huba na mengine ya kijamii.

Ingawa leo tofauti na siku nyingine, nina hasira na tashwishwi ya kusema na wanaume, namaanisha shemeji zenu, wapenzi wenu, wame zenu.

Wananikasirisha kiasi najiuliza wanakwamba wapi? Natamani niinue mikono juu kuashiria nimewashindwa.

Hizi dharau zinazowazunguka kuhusu kushindwa kulisakata samba zinatokana na nini. Mnashindwa kukutana wa mijini na vijijini mkajadili kwa pamoja nini haswa kimetokea?

Nimekasirika sana. Unakuta kijana jamali, lakini katulie naye mahali baada ya muda mnakuwa kama mmekwenda kwenye jumba la sinema namna anavyojishughulisha na masuala la muvi , mara za bongo, Nigeria na Ulaya.

Kitaulo kiunoni, kila saa anakivunga vizuri kuashiria mchezo umeishia hapo na akilivua anavaa suruali kwa ajili ya kukusindikiza.

Narudia tena nimechukia. Napata malalamiko kutoka kwa mademu wenu, wanasema mnawatia jazba jinsi mnavyowapapasa.

Au tukubaliane kama vipi muachane na suala hilo mfanye vitu vingine, kwa sababu ni kama limeshindikana, kuliko kumhangaisha mwanamke aliyejiandaa kwa ajili ya kukuondoa mawazo bora mbaki kama mapambo muwe mnatizamwa tu.

Maana mambo yamebadilika. Siku za nyuma mwanamke ndiyo alikuwa anaandaliwa sana, mwanaume anakuwa tayari muda wote, lakini siku hizi shemeji zangu, baba zangu mnahitaji maandalizi kuliko ya kunyonyoa bata. Maana bila kufanya hivyo hutaambulia kitu, baadhi yenu mmeridhika kabisa na mnajitahidi kusingizia hadi maradhi.

Baadhi yenu mmebadili hata maeneo ya kusisimuliwa, utasikia...ukinishika chuchu nafurahi...aagh jamani mnaniangusha shemeji yenu kwa sababu lawama zinakuja kwangu, nimechoka kulaumiwa.

Nataka kujua mnafanya lini kikao kulitafutia ufumbuzi suala hili, nami nihudhurie. Nimekasirika lakini kikaoni nitakuja niwaeleze maeneo mnayotakiwa kuyafanyia kazi. Yaani tuna vijana shupavu, wanapendeza, lakini likija suala la nguvu kazi ya kwenye sita kwa sita inakuwa taabu.

Niwaeleze wale wanaojisifu sana kuwa ni wataalamu nao bado ana shida, kwa sababu wangekuwa na utaalamu kama wanaojisifu sidhani kama malalamiko yangetapakaa kila kona ya mji. Kuna wakati unaogopa hata kuwa na rafiki mwanaume, kwa sababu siku si nyingi mawifi watamiminika kulalamika kuwa hawashibishwi chakula cha roho.

Narudia tena fanyeni kikao mjadili. Hivi mwanaume unaposhindwa kucheza samba unataka nini kwenye maisha.

Halafu nyinyi ndiyo huwa mnasema ukikosa kucheza samba bora kufa, lakini hamfanyi kitu kumaliza hizi lawama kuwa mkiwekwa kwenye 18 mnambwela.

Acheni hizo bwana fanyeni jukumu lenu la kimaumbile inavyostahili. Kutaneni na wazee wawaeleze wao walikuwa wanafanya nini hadi wanaitafuta alfajiri wakiwa pamoja na wenza wao kiroho safi.

Nimechafukwa sana jamani.