Zahera: Kumkataa Mkwasa sababu ya kufukuzwa kwangu Yanga

Muktasari:

Uongozi wa Yanga umeachana na Zahera baada ya kuiongoza timu hiyo kwa msimu mmoja akiwa ameisaidia kumaliza nafasi ya pili katika Ligi Kuu Tanzania Bara

Dar es Salaam. Aliyekuwa kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera ameibuka na kusema sababu ya kutimuliwa kwake ni kukataa kufanya kazi Charles Mkwasa.

Akizungumza na redio EFM asubuhi leo Zahera alisema viongozi wa Yanga na mwenyekiti walikuwa wamemuhakikishia kuendelea na jukumu hilo kabla ya uamuzi wake wa kukataa kufanya kazi na Mkwasa kama msaidizi wake.

“Kusema ukweli Mwenyekiti aliniambia hata tukifungwa Misri hiyo siyo tatizo nitaendelea kuwa kocha.”

Zahera alisema najua sababu ya kufukuzwa kwangu ni kukataa kufanya kazi na kocha Mkwasa kama msaidizi wangu.

“Nilikuwa nimefanya naye mazungumzo ya mambo yote kabla, lakini tatizo ni kukataa kufanya kazi na Mkwasa,” alisema Zahera.

Uongozi wa Yanga jana ulimtangaza Mkwassa kuwa kocha wa muda wa Yanga kuchukua jukumu la Zahera hadi watakapopata kocha wa kudumu.

Dk Msola alisema wameamua kufikia hatua ya kuvunja mkataba Zahera baada ya kukaa na kuzungumza na pia kuona Mkwasa anafaa kuishika timu hiyo kwa muda baada ya kuachana na kocha wao.

"Mkwasa ndio atakayekuwa na timu hii kwa muda wa takribani wiki mbili wakati huo tukiangalia kocha wa kudumu, pia Mkwasa hatoweza kukaa peke yake kwahiyo tutakaa naye na kujua atakuwa na nani," alisema.

Mkwassa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Yanga alijiondoa katika nafasi hiyo kutokana na kusumbuliwa na maradhi.

Akizungumzia suala la afya ya Mkwasa, Msola alisema "Mpaka tumefikia hatua hii maana yake Afya yake ni nzuri, lakini sio jambo sahihi kulizungumzia hapa."

Mkwasa atakuwa akisaidiwa na winga wa zamani wa Yanga, Said Maulid ‘SMG’ aliyekuwa kocha wa timu ya vijana.