Wanyama huyu huyu kuwa mlami

Muktasari:

Wanyama alihamia Uingereza akitokea Celtic ya Scotland, alipisajiliwa na Southamption na baada ya misimu minne akajiunga na Tottenham

STORI iliyopo kwa sasa ni kiungo Victor Wanyama muda wote kuanzia sasa atageuka na kuwa mlami, yaani mzungu.

Nahodha huyo wa Harambee Stars, Wanyama yupo mbioni kuchukua uraia wa Uingereza baada ya kuishi nchini humo kwa miaka sita.

Kulingana na jarida la Daily Mail, Wanyama anayekipiga katika klabu ya Tottenham Hotspurs aligomea uhamisho ambao ungemtoa Uingereza msimu uliopita.

Hii ni kwa sababu alitaka kuhakikisha anatimiza masharti yote yanayotakiwa kwa raia ya nchi ya kigeni kupata uraia wa taifa hilo.

Uamuzi huo ulihakikisha Wanyama anatimiza miaka sita ya kuishi na kufanya kazi Uingereza, sharti linalotosha kumpa uraia wa taifa hilo.

Sasa taarifa ni kwamba wiki hii muda wowote, Wanyama atapokea pasipoti yake ya Uingereza itakayomfanya kuwa raia wa mataifa mawili Uingereza na Kenya.

Hii ina maana Wanyama atakuwa na uwezo wa kusafiri katika mataifa ya Ulaya bila ya kuhitaji kuwa na Visa.

Huku hayo yakijiri, muda wake pale Tottenham unasemeka umefikia kikomo na huenda akaondoka muda wowote hasa baada ya klabu hiyo kufanikisha usajili wa kiungo mkabaji Tanguy Ndombele kutoka Lyon anayecheza nafasi moja na Wanyama.

Msimu uliopita Wanyama alikumbwa na mkosi wa jeraha la goti ambalo lilimsumbua sana na kumsababishia kukosa muda wa kutosha wa mchezo jambo ambalo limepelekea benchi la ukufunzi kutafuta mbadala wake.

Jarida hilo limeripoti huenda Wanyama akaondoka kabisa Uingereza na kuhamia kwingineko Ulaya baada ya klabu za nchini humo kutoonyesha nia ya kuhitaji huduma zake.

Wanyama alihamia Uingereza akitokea Celtic ya Scotland, alipisajiliwa na Southamption na baada ya misimu minne akajiunga na Tottenham.

 Ishu ya Wanyama kuchukua uraia wa kigeni wala sio ishu jipya. Miaka miwili iliyopita, kipa wa zamani chaguo la kwanza wa Harambee Stars, Arnold Origi alitangaza kustaafu soka la kimataifa baada ya kupata uraia wa taifa la Norway.

Binamuye huyo fowadi wa Liverpool Divorck Origi, kaisha Norway kwa zaidi ya miaka 12 akicheza soka lake huko. Pia ndio ndio muda aliotumikia Stars. Hata hivyo aliamua kustaafu 2017 baada ya kufanikiwa kupewa uraia wa taifa hilo.