Nahodha Njombe Mji akili ugeni tatizo

Muktasari:

  • Njombe Mji imecheza kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Uhuru tangu kupanda Ligi Kuu Bara

Dar es Salaam. Nahodha wa Njombe Mji, Laban Kambole amesema uzoefu mdogo wa ligi umechangia kupata kipigo cha mabao 4-0 kutoka kwa Simba jana kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Kambole alisema Simba ni timu kubwa tofauti na wao ambao wamepanda daraja msimu huu na kucheza Ligi Kuu kwa mara ya kwanza mwaka huu.

"Timu yetu wachezaji wengi ni wachanga na ukweli tulizidiwa katika mchezo huo kwani wengi hawana uzoefu wa ligi."

"Tatizo kubwa la wachezaji wengi wa Tanzania huwa tunaogopa majina ya hizi timu hivyo unakuta ukifika uwanjani unasahau kufanya uliyoelekezwa na kucheza unavyojua wewe," alisema Kambole.

Kambole alisema bado wana nafasi ya kufanya vizuri katika michezo mingine ijayo kwani wanachoshukuru wameshamaliza kucheza na Yanga na Simba kwenye mzunguko wa kwanza.

"Tumeshacheza na Yanga na Simba hivyo sasa tutashusha presha na kupambana katika michezo ijayo kuhakikisha haturudi tulikotoka," alisema nahodha huyo ambaye timu yake ilicheza kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Uhuru.