Unai Emery kwenye namba mambo yake si haba!

Muktasari:

Safari hii, Freddie Ljungberg, ndiye aliyekuwa kwenye benchi la ufundi, akiwa kocha mkuu mpya wa kipindi cha mpito.

LONDON, ENGLAND .DAKIKA 90 za kwanza ilizocheza Arsenal kwenye Ligi Kuu England bila ya huduma ya Unai Emery kwenye benchi hazikuwa na mabadiliko yoyote ya maana zaidi ya mechi saba za mwisho za Mhispaniola huyo huko Emirates.

Emery alifutwa kazi baada ya kushindwa kupata ushindi wowote kwenye mechi saba mfululizo. Ameondoshwa na mechi iliyofuata, Arsenal walicheza na Norwich City, wanaopambana wasishuke daraja, hakukuwa na jipya, Arsenal walihitaji bao la kusawazisha na Pierre-Emerick Aubameyang kujiokoa kwenye kipigo na kutoka 2-2.

Safari hii, Freddie Ljungberg, ndiye aliyekuwa kwenye benchi la ufundi, akiwa kocha mkuu mpya wa kipindi cha mpito.

Kocha Emery katika mechi 51 alizoisimamia Arsenal, ameshinda 25, akatoka sare 13 na kupoteza mara 13 huku akivuna pointi 88. Hazikuwa rekodi mbaya, lakini shida ni kwamba Arsenal matarajio yao yalikuwa tofauti zaidi.

Kwa ujumla wake, Emery ameinoa Arsennal kwenye mechi 78, ameshinda mara 43, sare 13 na kupoteza mara 19, akiwa na wastani wa ushindi wa asilimia 55.1. Hakuna taji alilobeba baada ya msimu uliopita kuchapwa kwenye fainali ya Europa League. Kabla ya kujiunga na Arsenal, Emery ni sehemu moja tu ambayo alifanya kazi na hakubeba taji. Ni Valencia, mahali ambalo aliongoza wkenye mechi 220, akishinda 107, sare 58 na kupoteza mara 55 huku akiwa na wastani mdogo zaidi wa ushindi, asilimia 48.6. Lakini, muda wake aliokuwa Sevilla na Paris Saint-Germain ndio uliowashawishi mabosi wa Arsenal na kumchukua akafanye kazi kwenye timu yao baada ya Arsene Wenger kuondoka.

Huko Sevilla, Emery aliongoza kwenye mechi 205, akishinda mara 106. Ametoka sare 43 na kupoteza mara 56. Aliondoka hapo alibeba mataji matatu, yote ya Europa League. Hiyo iliwavutia PSG na kwenda kumpa kazi kwenye timu yao, ambayo aliwaongoza kwenye mechi 114, akishinda 87, sare 15 na kupoteza mara 12 tu. Mahali hayo alikuwa na wastani wa ushindi wa asilimia 76.3 huku akiondoka na nafasi yake kuchukua Thomas Tuchel baada ya kubeba mataji saba.

Kwa jumla yake kwenye timu hizo nne vigogo wa huko Ulaya, Emery amesimamia katika mechi 617 na kuibuka na ushindi katika mechi 343, ikiwa ni zaidi ya nusu ya mechi zake zote. Kwenye namba tu, Emery mambo yake si haba.