Ukipanga matokeo mechi za mchujo imekula kwako

Muktasari:

Kuelekea mechi za play-off zinazochezwa leo katika viwanja tofauti, TFF imetoa onyo kali kwa waamuzi na viongozi kuepukana na hujuma ambazo zitaondesha haki.

UHAKIKA wa Mbeya City na Mbao FC, kubaki Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL) au kushuka, utaanza kuonekana kuanzia leo Jumatano Julai 29, 2020 kwenye mechi zao za mchujo zitakapocheza na timu zilizomaliza nafasi ya pili Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

Mbeya City itakuwa mgeni wa Geita, Mbao FC nayo itacheza ugenini dhidi ya Ihefu, kuelekea mechi hizo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limetoa onyo kuhakikisha mechi hizo zinachezeshwa kwa haki.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisa Habari wa TFF, Cliford Ndimbo imesema waamuzi ama viongozi wa timu hizo atakayebainika kufanya vitendo vya hujuma watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Amesema TFF itafuatilia kwa ukaribu matukio yote katika mechi hizo, kuhakikisha kila timu inapata haki inayostahiki.

"Mechi hizo zitaonyeshwa moja kwa moja kupitia Azam Tv, hivyo yatafuatiliwa matukio yote, kuhakikisha timu inapata stahiki inayotakiwa,"

"Hatua hizo zitachukuliwa kwa mujibu na taratibu zinazoendesha mpira wa miguu,"amesema.