Tshabalala aahidi raha Simba

Muktasari:

Simba inashika nafasi ya kwanza katika msimamo wa Ligi Kuu ikiwa na pointi 71 na inahitajika kupata ushindi katika mechi tano kati ya 10 ilizobakiza ili itwae ubingwa.


NAHODHA msaidizi wa kikosi cha Simba, Mohammed Hussein 'Tshabalala' amesema wamejipanga kuhakikisha wanaendelea pale walipoishia kile katika Ligi Kuu Bara na Kombe la Shirikisho la Azam.

Tshabalala alisema waliishia na moto wa kufanya vizuri katika ligi kwa maana ya kupata matokeo mengi ya ushindi na hilo ndio wamejipanga kama wachezaji kwenda kuliendeleza.

Alisema katika mazoezi wanapewa mafunzo, mbinu ma maelekezo kutoka kwa makocha wao lakini jukumu kubwa linabaki kwa wachezaji kwenda kuyafanyia kazi hayo yote katika mechi husika.

"Kimsingi kama wachezaji tumekaa na kutambua tupo na jukumu kubwa la kutimiza malengo ya timu ambayo ni kuchukua ubingwa wa ligi na Kombe la Shirikisho la Azam.Hilo halitawezekana bila kushinda mechi zilizokuwa mbele yetu.

"Kwa aina hii ya maandalizi ambayo tunaendelea nayo nadhani tuna kila sababu ya kufanya vizuri katika mechi zetu ambazo tumebaki nazo na kama vile ambavyo tulifanya mwanzo wa msimu.

"Kikubwa tunaomba nguvu ya mashabiki wetu waendelea kujitokeza uwanjani kwani wachezaji wote tupo tayari kupambana kwa ajili yao na kuwapatia kile ambacho wanahitaji kutoka kwetu," alisema Tshabalala.