TFF yakomalia ligi ya wanawake

SHIRIKISHO la Soka Nchini (TFF) limefichua kuwa, limeanza mkakati wa kuzalisha fursa kwa wanawake ili kuendeleza soka la jinsi hiyo nchini.

Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao ndiye aliyefichua hayo alipozungumzia mafunzo ya Utawala na Uongozi kwa Wanawake inayofanyikia mkoani hapa.

Kidao alisema, soka la wanawake bado lina changamoto nyingi ambazo wameamua kuwekea mpango mkakati wa kuzitatua ikiwemo uhaba wa wachezaji, makocha na waamuzi wa kike sambamba na viongozi kuanzia ngazi ya klabu hadi shirikisho la Taifa.

“Mafunzo haya ni muendelezo wa mpango mkakati wa TFF chini ya Rais Wallace Karia ya kuendeleza soka la wanawake na kuzalisha fursa nyingi kwao hata kwa nafasi za kimataifa kama wanavyonufaika Kenya na Uganda.”

Alisema, mafunzo hayo ya utawala na uongozi yanafanyika nchi nzima ili kuwaonyesha wanawake fursa zilizoko katika soka, lakini pia kuwahamasisha kuzichangamkia.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Chama cha Soka Mkoa wa Arusha (ARFA), Zakayo Mjema alisema jumla ya walimu 30 wananufaika na semina hiyo ya wiki moja kutoka wilaya zote kwa wanawake na wanaume.”