Prince Dube aishi kifahari dar, aiponza Yanga

MWANASPOTI linajua vigogo walio karibu na Yanga wamempa maisha ya kifahari staa anayepambana kuvunja mkataba na Azam, Prince Dube lakini klabu imeingia msituni kwa staili ya tofauti.

Dube kwa sasa anaishi kwenye jumba moja la kifahari maeneo ya Salasala, Dar es Salaam kilomita chache kutoka kwenye ufukwe wa bahari ya Hindi.

Lakini habari za ndani ambazo Mwanaspoti inazo ni kwamba Azam imeshashtukia dili kwamba baadhi ya watu wa karibu wa Yanga wapo ndani ya sakata la dube kusitisha mkataba na wao wameamua kurivenji.

Habari zinasema kwamba azam wamepania kuitingisha Yanga kupitia kwa baadhi ya mastaa wake ambao mikataba yao inaelekea ukingoni lakini watang'oa mmoja wao Clement Mzize akiwemo.

Azam wanadai wameshapeleka ofa ya Sh 400 milioni kwa Yanga lakini hawajajibiwa lakini wana uhakika kwamba staa huyo mkataba wake unamalizika mwisho wa msimu huu.

Kwa upande wa Dube

Iko hivi, Yanga inaelezwa kuwa imelipa kisasi kwa timu hiyo baada ya Azam kumchukua kiungo wake Feisal Salum ‘Fei Toto’ msimu uliopita, nayo sasa imemuandalia mkataba wa miaka miwili mshambuliaji huyo.

Dube aliyeifungia Azam mabao sita msimu huu, kwenye ligi aligoma kurejea klabuni hapo akishinikiza kuondoka kwa madai hana furaha na klabu hiyo iliyomleta nchini miaka minne iliyopita na hivi karibuni alionekana akiwa kwenye majukwaa ya Uwanja wa Benjamin Mkapa analindwa na mabodigadi kila upande akishuhudia mechi ya Azam ambayo ilishinda 2-1 dhidi ya Yanga.


Baada ya Dube kujiondoa kikosini akawafuata Azam akitaka kulipa fedha ili anunue mkataba wake huku matajiri hao wa Chamazi wakigomea kiasi hicho cha dola 150,000 na kutaka dola 300,000 sawa na zaidi ya Sh700 milioni.

Hata hivyo, kesi hiyo imetinga TFF lakini bado hawajatoa tamko rasmi ya kilichofikiwa kwenye kikao cha hivi karibuni.

Taarifa za uhakika ambazo Mwanaspoti inazo ni kwamba Dube tayari ameshaandaliwa mkataba wa miaka miwili na Yanga ukiwa na maslahi ya kutosha.

“Dube ameandaliwa mkataba na Yanga, nadhani ndio klabu anayoitaka kuichezea hapo Tanzania, mkataba una vipengele vingi, kuna nyumba, gari lakini mshahara nao ni mnono sana, Azam wangemuacha tu kwani tayari wameshampa mkataba na hana furaha na maisha ya Azam.

“Ukiongea naye anakuwa mkali sana hataki kuisikia Azam wala klabu yoyote, ukiongea anasema anataka kucheza klabu ambayo ina tabia ya kuchukua makombe kwani anataka kuwa na mafanikio kokote anakokwenda,” alisema mmoja wa marafiki wa mshambuliaji  huyo anayecheza nchini.

Inaelezwa walinzi waliokuwa wakimlinda Dube hivikaribuni wanatoka kwenye kampuni moja kubwa ya ulinzi binafsi (jina tunalo), inayomilikiwa na kigogo wa Yanga