Sturridge kampata yule mbwa wake buana

Muktasari:

Video na picha za mbwa huyo zilichapishwa mitandaoni na baada ya hapo akarejeshwa kwa mmiliki wake halali.

LIVERPOOL, ENGLAND.STRAIKA aliyemaliza mkataba wake Liverpool, Daniel Sturridge ameelezea furaha yake baada ya kumpata mbwa wake aliyepotea aitwaye Lucci.
Sturridge, 29, alitangaza dau la kufikia Pauni 40,000 (Sh. 92 milioni) kwa yeyote ambaye angemletea mbwa huyo ambaye alipotea baada ya nyumba yake ya Marekani kuvunjwa na wezi.
Video na picha za mbwa huyo zilichapishwa mitandaoni na baada ya hapo akarejeshwa kwa mmiliki wake halali.
"Siamini," Sturridge alisema katika video aliyoposti kwenye ukurasa wake wa Instagram.
"Nataka tu kusema asante kwa kila mtu mitandaoni aliyeniunga mkono na kupaza sauti. Ninashukuru sana."
Hata hivyo, Sturridge hakusema kama alitoa pesa alizoahidi kwa mtu aliyemrejesha mbwa huyo.
Baada ya mkataba wa Sturridge kumalizika Liverpool, mchezaji huyo wa kimataifa wa zamani wa England, huenda akajiunga na Aston Villa iliyorejea kwenye Ligi Kuu ya England.