Staa Madrid atoroka karantini kufuata demu

Muktasari:

Amesababisha mijadala mizito nchini Serbia na baba yake, Milan Jovic, amezungumzia jambo hilo.

MADRID, HISPANIA . BABA wa Luka Jovic amesema ni lazima mwanaye aikubali adhabu yoyote atakayopewa kwa kutoroka karantini na kwenda mjini Belgrade.

Straika huyo wa Real Madrid amekosolewa kwa kusafiri hadi Serbia kusherehekea ‘bethidei’, ya rafikiye wa kike wakati alipaswa kuwa nyumbani kutimiza kanuni ya siku 14 za kukaa karantini.

Amesababisha mijadala mizito nchini Serbia na baba yake, Milan Jovic, amezungumzia jambo hilo.

“Luka alifanyiwa vipimo (vya virusi vya Corona) mara mbili na mara zote ameonekana hana,” Milan Jovic alifafanua.

“Ndio maana alidhani kwamba anaweza kuja Serbia.

“Sasa linaonekana ni kosa kubwa la jinai.

“Kama atahukumiwa kwenda jela, ataenda.

“Naungana kikamilifu na Rais wa Serbia na Waziri Mkuu (kwa kutishia mashitaka ya jinai), lakini tu kama atakutwa na hatia.

“Nitasapoti uamuzi huo iwapo atabainika amefanya jambo lolote baya, lakini aliwasili Belgrade na hakutoka ndani.

“(Rafikiye wa kike) Sofia ni mjamzito na asingeweza kwenda kwenye mtoko (kusherehekea siku yake ya kuzaliwa).

“Baadhi ya picha zimezagaa zikiwaonyesha wawili hao wakiwa katika mtoko wakifurahia maisha, lakini ukweli ni kwamba picha hizo zilipigwa wakati wakiwa Hispania.”